Friday, March 14, 2008

BOT sasa yaiogopa EPA!

Baada ya moto uliowaka sasa inaonekana kuwa akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) ni moto kweli kweli na Benki Kuu imeonyesha dhamira ya kutaka kujitoe kuendesha akaunti hiyo.

Gavana wa BoT, Benno Ndulu amesema leo kuwa tayari BoT imeshawasiliana na mtaalamu, ambaye ni kampuni moja kutoka nchini kutoka nchini Ufaransa, ili aje kufanya tathmini itakayosaidia kuamua iwapo akaunti hiyo iendelee kubaki BoT au la.

Lakini Ndulu amesema kuwa kimsingi, EPA si sehemu ya shughuli za BoT na ndio maana wanataka kuiondoa akaunti hiyo chini yao.

Gavana Ndulu amesema kuwa kampuni hiyo itatakiwa kukamilisha kazi yake kabla ya katikati ya mwaka huu ili uamuzi wa wapi akaunti hiyo iwekwe ufanywe. Inaonekana kuwa lengo lake ni kuhakikisha kuwa unapoanza mwaka mpya wa fedha mwezi Julai, shughuli za akaunti hiyo zikabidhiwe kwa taasisi inayostahili kuiendesha.

Awali, kabla ya kuhamishiwa BoT, akaunto hiyo ilikuwa ikiendeshwa na NBC.

Baada ya kuhamishiwa BoT, wajanja wachache, kwa kutumia nyaraka za kughushi na ulaghai, walichota kisi cha sh bilioni 133 kutoka katika akaunti hiyo.

Wizi huo ulibainishwa na wanasiasa, hasa wa upinzani walipozungumza bungeni, ingawa viongozi wa serikali walijipanga kukanusha.

Hata hivyo, mbinyo wa wapinzani uliendelea hadi serikali kulazimika kuialika kampuni ya kimataifa ya ukaguzi wa hesabu wa Ernst & Young ambayo mwishoni mwa mwaka jana ilithibitisha kuwa kweli wajanja wamejichotea mabilioni kutoka katika akaunti hiyo.

No comments: