Tuesday, November 6, 2007

Haya Ndiyo Mashitaka ya Dalali wa Rada

Mnaweza kuwa mmesikia kuwa yule bwana mkubwa aliyekuwa mtu wa kati katika deal ya ununuzi wa rada amefunguliwa mashitaka na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (TAKUKURU). Lakini mnaweza kuwa hamjapata mashitaka halisi yanayomkabili bwana mkubwa huyo.
Nimebahatika kuiona hati ya mashitaka (Charge sheet) yanayomkabili, na nimeamua kuiweka hapa kwa tafsiri yake ambayo si rasmi (yenyewe imeandikwa kwa kiingereza na nimeacha mambo kadhaa ambayo nimehisi si ya msingi na hayabadili maana sana yaliyomo).
Inasomeka ifuatavyo;

KOSA LA KWANZA
Perjury (hii ni lugha ya kisheria wala sijui maana yake nini)
Kinyume na kifungu 102 cha kanuni ya adhabu.

MAELEZO YA KOSA
SHAILESH PRAGJI VITHLAN, mnamo Jumatano Julai 25, 2006, ulipokuwa mbele ya Hakimu Mkazi Katarina Revocati katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wilayani Ilala katika mkoa wa Dar es Salaam, ukitoa ushahidi kwa mujibu wa sheria, wakati ukifahamu, ulitoa ushahidi ambao si kweli kuhusiana na suala la serikali ya Tanzania kununua rada iliyoigharimu USD 39,972.450 kuwa ENVERS TRADING CORPORATION ilikuwa inamilikiwa na Pablo J. Espino na Adelina M. Estriby, jambo ambalo si kweli kwa sababu kampuni hiyo ilikuwa chini ya umiliki wake (Vithlan) kama mkurugenzi na alilipwa asilimia 31 ya bei ya rada ambayo ni sawa na USD 12,391,459 kama kamisheni ya kile kilichoitwa kuwa ni ushauri kwa mujibu wa mkataba kati ya RED DIAMONG TRADING CORP na ENVERS TRADING CORP.

KOSA LA PILI
Chini ya kidungu hicho hicho kilichotajwa hapo juu.

MAELEZO YA KOSA
SHAILESH PRAGJI VITHLAN, manmo Julai 28, 2006 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akiwa katika kiapo, alitoa ushahidi wa uwongo kwamba alilipwa na British Aero Space System (Bae System) USD 390,000 tu ambazo ni sawa na asilimia moja ya bei ya rada iliyonunuliwa na serikali ya Tanzania kutoka Bae Sysytem kama malipo ya ushauri alioutoa kwa kampuni hiyo.

KOSA LA TATU
Kusema uwongo mbele ya afisa wa serikali

MAELEZO YA KOSA
SHAILESH PRAGJI VITHLAN, mnamo Desemba 27 katika hoteli ya Sea Cliff, Dar es Salaam alimueleza KASSIM EPHREM ambaye ni afisa mwandamizi wa TAKUKURU kuwa yeye (Vithlan) alikuwa amelipwa asilimia moja tu ya bei ya rada kutoka Bae System, kauli ambayo alifahamu kwa si kweli na aliitoa kwa lengo la kuathiri upelelezi uliokuwa unaendeshwa na KASSIMU EPHREM kuhusiana na taratibu za ununuzi wa rada.

***********
Hati inaonyesha kuwa mashitaka yalifunguliwa Novemba Mosi, 2007 na hii ni kesi ya jinai iliyopewa namba 1474 ya mwaka 2007 na wala aihusiani na uhujumu uchumi au rushwa.

No comments: