Sunday, December 30, 2007

Raila Alonga

Mgombea wa ODM, Raila Odinga, ameitisha mkutano waandishi wa habari asubuhi hii na kuitaka tume ya uchaguzi (ECK) kuacha kutangaza matokeo ambayo anadai yamepikwa.

Katika mkutano huo, Raila aalimtaka mwenyekiti wa tume hiyo, Samuel Kivuitu, kujiuzulu wadhifa wake kuliko kukubali kutumika kumuweka mtu madarakani kwa hila.

Lakini inashangaza kuwa raila amesema hawezi kwenda mahakamani kupinga yale anayoyaona kuwa ni kasoro. Anataka kufanya nini?

Raila anaamini kuwa matokeo ya baadhi ya maeneo yalifichwa makusudi ili kuokoa kahazi kwa rais Mwai Kibaki katika mazingira kama yaliyotokea.

Aliyataja baadhi ya majimbo ambayo yalificha matokeo kwa ajili hiyo kuwa ni Juja, Nithi, Maragua, Kiambaa na Gatanga, ambayo yana wafuasi wengi wanaomuunga mkono Kibaki.

Pia kuna tofauti kubwa kati ya idadi ya kura zilizotangazwa na ECK na matokeo ambayo ODM imeyapata kutoka kwa wasimamizi wake katika baadhi ya vituo. Akitoa mfano, raila alisema ECK inasema huko Juja, Kibaki amepata kura 78,000 wakati mawakala wa ODM wanaonyesha kuwa kura aliziopata Kibaki ni 52,000 tu.

Pia matokeo ya ECK yanaonyesha kuwa katika baadhi ya vituo, idadi ya watu waliojitokeza kupiga kura ni zaidi ya asilimia 100 ya watu waliojiandikisha.

Raila sasa anaitaka ECK kupitia upya, matokeo yote iliyoyatangaza. Mpaka kazi ya kutangaza matokeo inasitishwa jana jioni, takwimu za ECK zilikuwa zikionyesha kuwa raila alikuwa anaongoza kwa kura 3,880,053 dhidi ya kura 3,842,051 za Kibaki.

No comments: