Monday, March 31, 2008

Mashaka Yaanza Zanzibar

Kile kilichokuwa kikihofiwa siku zote, sasa kinaweza kutokea. Hali ya mambo kisiwani Zanzibar imeanza kuwa ya wasi wasi kutokana na maamuzi yaliyofikiwa katika kikao cha NEC ya CCM huko Butiama.

Kinachoonekana kikuweka rehani kisiwa hicho ni kukengeuka kwa CCM na kuamua kupindisha kilichokubaliwa katika kamati ya Mazungumzo na kutaka ifanyike kura ya maoni kuhusu kuanzishwa kwa serikali ya Mseto visiwani humo.

Katika kile kinachoashiria kuwa hali ya mambo imeanza kuwa mbaya, wajumbe wa Baraza la wawakilishi wa CUF, waliacha kuendelea na vikao vya baraza na kwenda katika makao makuu ya chama chao ambajko ulifanyika mkutano.

Habari kutoka ndani ya chama hicho zinaeleza kuwa wajumbe hao wametakiwa na wanachama wao kususia vikao vyote vya baraza la wawakilishi.

Aidha, kuna taarifa pia kuwa wanaCUF wamewataka wabunge wao kutohudhuria vikao vya Bunge, linalotarajia kuanza kukutana mjini Dodoma wiki ijayo.

Wajumbe hao wa CUF walitoka Barazani wakiongozwa na Mnadhimu wa kambi ya upinzani, Soud Yussuf Mgeni, muda mfupi baada ya kipindi cha maswali na majibu kumalizika.

Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Umma na Haki za Binaadamu wa CUF, Salum Bimani alisema kwamba kikao hicho kiliitishwa baada ya viongozi wa chama na wajumbe wa Baraza hilo kupewa ujumbe wa simu kutoka kwa wanachama kuwataka wasusie mara moja vikao vya Bunge na Baraza la Wawakilishi.

Tayari watu kadhaa wameshaanza kuonyesha wasi wasi wao kutokana na maamuzi yaliyofikiwa na CCM , ambayo yabnaonekana kurudisha nyuma hatua iliyokubaliwa na Kamatio ya Mazungumzo ambayo iliwashirikisha wajumbe kutoka CCM na CUF.

Katika mazungumzo hayop, ilikubaliwa kuwa iundwe serikali ya mseto Zanzibar, ambapo chaka kitakachoshinda uchagzui kitatoa rais na kile kinachofuatia kitatoa waziri Kiongozi.

Lakini suala hili limekuwa likipingwa miaka yote ya wahafidhina walio ndani ya CCM Zanzibat na wamejiapiza kuwa kamwe hawatoiruhusu CUF katika serikali yao.

Biomani alisema kuwa CUF kimepokea maamuzi ya NEC lakini kitatoa maamuzi yake Jumanne kupitia mkutano na waandishi wa habari, ambao utahutubiwa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Sharif Hamad.

Wakati huo huo, uamuzi wa NEC ya CCM kuwa suala hilo liamuriwe kupitia kura ya maobni, limezua mjadala visiwani hapa, huku baadhi ya watu wakipinga wazo hilo.

Katibu wa TADEA, Juma Ali Khatib, alisema suala la kuitisha kura ya maoni juu ya serikali ya pamoja visiwani humu si muafaka kwa sasa kwa sababu muda uliobakia ni mdogo.

Alieleza kwamba Kamati ya Mazungumzo ya CCM na CUF ilipaswa kulitambua hilo mapema, kwa vile linagusa katiba na sheria za uchaguzi.

Naye Mkurugenzi wa Habari wa NCCR-Mageuzi, Ali Omar, alisema kwamba wakati muafaka umefika kwa Rais Jakaya Kikwete kutangaza kuwa ameshindwa kutatua mpasuko wa kisiasa wa Zanzibar.

Alisema kwamba kwa kuzingatia kuwa suala la serikali ya mseto linahusu maslahi ya taifa halikupaswa kurejeshwa kwa wananchi kwa vile hatua hiyo ni sawa na kupoteza muda.

“NCCR-Mageuzi tunavyoona Rais Kikwete ameshindwa kutekeleza ahadi yake ya kumaliza mpasuko wa kisiasa kama alivyoahdi katika Bunge,” alisema kiongozi huyo.

mwisho

No comments: