Tuesday, April 8, 2008

BREAKING NEWS: Wabunge wa upinzani watoka Bungeni

Bunge limeanza asubuhi hii kwa wabunge wa upinzani kutoka ndani ya Bunge wakipinga kile walichokitaja kuwa ni kusuasua kwa mazungumzo ya kusaka suluhu ya mpasuko wa kisiasa Zanzibar.
Wabunge hao walisimama na kutoka baada ya kuapishwa kwa wabunge wawili wapya, ole Nangaro aliyechaguliwa hivi karibuni katika uchaguzi mdogo wa jimbo la Kiteto na Al-Shaimaa John, mbunge wa kuteuliwa.
Baada ya kuapishwa kwa wabunge hao, wakati Spika alipomuita Waziri wa Nchi, Philip Marmo kuwasilisha hati mezani, wabunge hao walisimama na kuanza kutoka, jambo lililowafanya wabunge wengine kupiga makofi.
Hapo Spika alimsimamisha Marmo na kumtaka atulie kwanza ili ‘tukio’ hilo lipite. Walipotoka na hali kutulia, Spika alisema kuwa asubuhi, Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Hamad Rashid Mohamed, alikwenda nyumbani kwake na kumtaarifu kuwa wabunge wa upinzani watatoka kabla ya kipindi cha maswali na majibu kupinga kusuasua kwa mqazungumzo ya kusaka suluhu ya mpasuko wa kisiasa Zanzibar.

No comments: