Wednesday, April 9, 2008

Msimamo wa CUF kuleta mabadiliko Bungeni

UPO uwezekano mkubwa wa kanuni za Bunge kubadilishwa au kuongezwa nyingine, kutokana na kitendo cha wabunge wa Chama cha Wananchi (CUF) kususia kikao cha ufunguzi cha Bunge juzi.
Spika wa Bunge, samwel Sitta, alikiri jana kuwa kitendo hicho cha wabunge wa CUF kimebainisha kuwepo kwa kasoro katika kanuni za Bunge.
Spika alibainisha kuwa baada ya kutokea kwa tukio hilo, alipata ushauri wa watalaamu wa sheria. Alisema bado wanaliangalia suala hilo lakini ushauri aliokwishapatiwa unaonyesha kuwepo kwa upungufu wa kikanuni kuhusiana na suala hilo.
Alisema iwapo italazimu, kanuni zitabadilishwa au kuongezwa, ili kukabili hali kama hiyo inapojitokeza.
Aidha, Spika alisema ni lazima kanuni za Bunge ziangaliwe upya kwa sababu kwa mtazamo wake, haoni ni jinsi gani suala la mazungumzo ya CCM na CUF nje ya Bunge, yanaweza kulihusisha Bunge.
Kwa maana hiyo, alisema kuwa upo ulazima wa kuweka kanuni kwa namna ambavyo zitaweza kushughulikia tatizo kama hilo iwapo litajitokeza tena siku za usoni.
Akifafanua, alisema kuwa ipo hatari kuwa iwapo suala hilo litaachwa liendelee, hapo baadaye wabunge wa chama kingine wanaweza kutoka Bungeni kwa sababu tu wana mgogoro na chama kingine.
Upo uwezekano mkubwa kwa wabunge wa Chama cha Wananchi (CUF) waliosusia vikao vya Bunge mjini Dodoma na kurejea kwenye chama chao kwa ajili ya kazi nyingine kunyimwa posho za siku ambazo hawatokuwepo Bungeni.
Hayo yalibainishwa na Spika wa Bunge, samwel Sitta, wakati alipokuwa akitoa ufafanuzi kuhusu hatua ya wabunge hao kuamua kuondoka baada ya juzi kususia kikao cha ufunguzi cha Bunge kutokana na kile walichokiita kuwa kukerwa kwao na kusuasua kwa mazungumzo ya kusaka suluhu ya mpasuko wa kisiasa Zanzibar.
Sitta alisema jana kuwa wabunge hao hawawezi kulipwa posho kwa sababu watakachokuwa wanakifanya wakati w akikao cha Bunge, hakihusiani na shughuli rasmi za Bunge.
Wabunge wa CUF, wakiungwa mkono na wengine kutoka vyama vya upinzani, juzi walitoka nje ya ukumbi wa Bunge, muda mfupi baada ya Spika kufungua kikao cha kwanza cha Mkutano wa 11 wa Bunge hilo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa Spika na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Hamad Rashid Miohamed, wabunge hao waliamua kuchukua hatua hiyo ili kuonyesha kutoridhishwa kwao na kusuasua kwa mazungumzo baina ya vyama hivyo.
Mazungumzo hayo yaliyochukua miezi 14 na kuelezwa kufikia hatua nzuri, yalichukua mtazamo mpya mwishoni mwa mwezi uliopita, pale CCM ilipotumia vikao vyake vya juu vilivyofanyika mkoani Mara, kubadilisha baadhi ya makubaliano, hasa yaliyohusu kuundwa kwa serikali ya mseto.
Wakati rasimu ya makubaliano hayo iliyosambazwa na CUF ikionyesha kuwa makubaliano yalikuwa ni kuundwa kwa serikali ya mseto mara moja baada ya kusainiwa kwa makubaliano hayo, rasimu ya CCM, iliyoweasilishwa kwenye kikao cha Kamati Kuu na NEC na katibu Mkuu, Yusuf Makamba, ilikuwa na pendekezo la kufanyika kwa kura ya maoni kuhusiana na uanzishwaji wa serikali ya mseto.

No comments: