Wednesday, April 23, 2008

HALI TETE UDSM

SERIKALI imetangaza kuwafutia udahili wanafunzi takribani 300 wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM) kutokana na vurugu zilizodumu kwa muda sasa chuoni hapo.

Uamuzi huo wa serikali ulitangazwa Bungeni na waziri wa Elimu na Mafunzio ya Ufundi, Profesa Jumanne Maghembe, ambaye alisema wanafunzi hao wamafukuzwa kutokana na kukiuka amri ya uongozi wa chuo hicho.

Akiwasilisha tamko la kuwafutia udahili wanafunzi hao jana jioni, Profesa Maghembe alisema kuwa miongoni mwa waliofutiwa udahili ni wanafunzi 39 ambao walikamatwa na Polisi katika vurugu ziliztokea chuoni hapo juzi.

Miongoni mwao, 38 jana walifikishwa mahakamani wakikabiliwa na kesi tatu tofauti.

Profesa Maghembe alisema kuwa pamoja na hao 39, pia wanafunzi wengine zaidi ya 250, ambao waliandamana juzi na jana na kugoma kuingia madarasani, nao wamefutiwa udahili.

Alisema kuwa inasikitisha kuwa wanafunzi hao walikaidi agizo lililotolewa na uongozi wa chuo kuwataka warejee madarasani na serikali haiwezi kuivumilia hali hiyo.

Wakati huo huo, wanafuzni 38 waliokamatwa juzi kutokana na vurugu hizo, jana walifikishwa mahakamani kwa tuhuma za kufanya vurugu chuoni hapo, kumjeruhi askari na mwenzao mmoja.

Wanafunzi hao ambao wamefunguliwa mashitaka matatu tofauti, walifikishwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya mahakimu watatu tofauti.

Mwendesha Mashitaka, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Charles Kenyela, aliwataja wanafunzi hao kuwa ni Mohamed Rashid (24), Blessas Lyimo (21), Mtaha Frank (24), Natanael Innocent (22), Kisendi Rashid (24), Rahel Chasaba (22), Ester Sanga (21), Lutandilo Hosea (22), Mgaya Risper (24) na Rose Casmir (21).

Wengine ni Lugome Claus Daud (25), Mbaraka Charles (23), Abdallah Selemani (23), Charles Peter (24), Kizito Prim (23), Deodatus Ngoti (28), Juma Athumani (25), Gabriel Gibson (23), Chogelo Gregory (22) na Mwankunga Edgar (25).

Wanafunzi wengine wametajwa kuwa ni Munish Hilary (22), Patrick Yesaya (22), Alex Manonga (22), Maliwa Nyasilu (22), Abrahamani Ephraimu (23), Bugumia Matiko (22), Mtandika Miraji Andrew (27) na Maige Emmanuel (24).

Wengine ni Masudi Salehe (20), Mdeme Ramadhan (23), Jalud Said (23), Lutaiwa Frenk (22), mwasyeba Anosisya (24), Shahamila Royald (23), Ahmad Masasi (22), Fimbo Yoseph Frednand (25), Halima Mfaume (23) na Stella Kambanga (24).

Katika kesi ya kwanza ambayo inawahusisha wanafunzi wote 38, Kamishna huyo Msaidizi wa Polisi alidai mbele ya Hakimu Hassan Makube kuwa juzi, muda usiofahamu katika eneo la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wanafunzi hao walikula njama ya kuwafanyia fujo wanafunzi wenzao na wahadhiri, kwa lengo la kusababisha uvunjifu wa amani.

Alidai siku hiyo hiyo majira ya saa 10:50 jioni katika eneo hilo la chuo walifanya vurugu kwa kuwazuia wanafunzi na wahadhiri kuingia madarasani na kuwachapa, hali iliyosababisha uvunjifu wa amani.

Katika kesi nyingine iliyopo mbele ya Hakimu Saidi Msuya, wanafunzi 13 kati ya hao wanadaiwa kuwa juzi, muda usiofahamia eneo la chuo hicho, waliwajeruhi wanafunzi waliokataa kuungana nao kufanya vurugu chuoni hapo.

Mwendesha Mashitaka alidai siku hiyo hiyo, washitakiwa na waliimjeruhi mwanafunzi mwenzao, Rashid Ally kwa kutumia fimbo na mawe na kumsababishia maumivu.

Katika kesi ya tatu iliyopo mbele ya Hakimu Euphemia Mingi, wanafunzi 11 wanadaiwa kumjeruhi Ofisa wa Polisi aliyekuwa kazini.

Mwendesha Mashitaka, alidai katika tukio hilo lilitokea juzi, saa 7.30 mchana, wanafunzi hao walimjeruhi Polisi mwenye namba E 8464 Konstebo Petro, aliyekuwa kazini na kumkata kwa chupa katika mguu wa kulia.

Washitakiwa wote hao walikana tuhuma hizo na baadhi yao kuachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti. Masharti hayo ni kuwa na dhamini wawili wa kuaminika. Kesi hizo zitatajwa Mei 6 mwaka huu.

Wakati hayo yakitokea, hali ya mgomo iliendelea jana katika maeneo ya UDSM, ingawa hakukuwa na vurugu kama juzi.

Hata hivyo, akizungumza chuoni hapo, Makamu Mkuu wa Chuo Profesa Rwekaza Mkundala, aliwakana wanafunzi waliogoma na kusema kuwa si wanafunzi wake.

Jana kutwa nzima wanafunzi hao walikusanyika nuje ya majengo ya utawala, huku askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) wakiwa wameweka kambi chuoni hapo wakiwa na zana zao tayari kwa lolote litakalotokea.

Pamoja na madai ya kutaka wenzao takribani 20 waliosimamishwa warejeshwe, jana waliongeza dai jingine, wakitaka wenzai 38 waliokamatwa juzi wakati wa vurugu, waachiwe.

Hali ilizidi kuwa ya wasiwasi baada Askari wa Kikosi cha FFU kurejea tena chuoni hapo wakiwa kwenye magari zaidi ya nane likiwemo moja la kurusha maji, ingawa hawakupambana na wanafunzi kama juzi.

Hadi jana jioni hapakuwepo dalili za maelewano ya kusitisha mgomo huo, huku habari zikienenezwa na wanafunzi kuwa kuna mwanafunzi mmoja alifariki dunia baada ya kuzidiwa na moshi wa mabomu.

Akijibu maswali ya waandishi baada ya kikao na ujumbe kutoka Comoro, Profesa Mukandala alikiri kuwa suala la mgomo huo ni kubwa, lakini hafikiri kukifunga chuo haraka bila kupata amri kutoka Serikalini, licha ya wanafunzi kukaidi amri iliyowataka waingie madarasani.

Alisema kuwa wanafunzi wanaogoma ni wale ambao wameshindwa kujilipia ada. Akifafanua, alisema kuwa awali wanafunzi hao walimwendea wakamuomba nafasi ya kujiunga chuo Kikuu kwa maelezo kuwa wataweza kujilipia wenyewe.

Alisema baada ya kufanya mazungumzo na wakuu wa vitivo, zikapatikana nafasi zaidi ya 400 na wanafunzi hao waliruhusiwa kujiunga kwa sharti la kujilipia wenyewe.

Hata hivyo, profesa Mukandala alisema kuwa baada kusoma kwa kipindi cha muhula mmoja, wanfunzi hao waligoma kuendelea kulipa ada na sasa wanashinikiza chuo kifungwe, jambo analopingana nalo.

“Sisi tusingependa kufunga chuo kwani tunafahamu kwani ni usumbufu mkubwa na hasara,” alisema.

Wakati akitoa madai hayo kwa upande mwingine wanafunzi walikuwa wakiandamana katika maeneo ya chuo hicho wakipaza sauti zao wakitaka uongozi wa chuo ujiuzulu na wale wenzao 38 waliokamatwa juzi na Polisi waachiwe, ili waungane kudai wenzao waliofukuzwa.

“Hatuwezi kuingia madarasani kama wanavyotaka hadi wawaachie na kuwarejesha wenzetu waliokamatwa bila hatia na Polisi, ili tusaidiane kuwadi haki,” alisisitiza mmoja wao.

Kelele za mayowe zilizidi kutawala eneo la utawala wa chuo baada kuenezwa taarifa kuwa kuna wanafunzi watatu wamefariki, akiwemo mmoja mjazito aliyeripukiwa na mabomu ya kutoa machozi.

“Dada yetu mpendwa wetu ameuawa bila hatia na wanafunzi wenzetu wamekamatwa bila kufanya ghasia… Mukandala damu isiyo na hatia inakulilia… jiuzulu,” lilisema bango moja lililobebwa na mwandamanaji.

Hata hivyo, madai ya kufariki kwa wanafunzi yalikanushwa na uongozi wa chuo kwa maelezo kuwa wanafunzi wanne na wafanyakazi wawili ndio walipata majeraha kidogo wakati wanakimbia na wote wametibiwa na kuruhusiwa kurejea nyumbani.

Alisema anayedaiwa kufariki, Neema Hamidu, yu hai lakini amepelekwa kwenye zahanati moja huko Mikocheni kwa ajili ya uchunguzi zaidi baada ya kushtuka kutokana kuwa na ujauzito.

Mwanafunzi huyo anakaa katika Hostel za Mabibo.

Pia Profesa Mukandala alikanusha tuhuma alizokuwa anaelekezewa kuwa yeye ni kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

“Ndugu zangu hata nafasi hii mimi sikuiomba, niliitwa nikafanyiwa usaili nikaonekana nafaa, wala sijawahi kuhudhuria mkutano wa CCM Butiama,” alisema Profesa Mukandala huku akisisitiza kuwa anaongoza chuo kwa kufuata kanuni na taratibu za chuo.

Licha ya wanafunzi hao kuendelea kusisitiza kuwa wataingia darasani ikiwa tu wenzao watarejeshwa, uongozi wa chuo hicho ulishikilia msimamo wao kuwa wanafunzi 14 kati ya 20 hawatareshwa chuoni na sita walianza kuhojiwa jana, akiwemo Waziri Mkuu wa serikali ya wanafunzi, Julis Mtatiro.

Kwa upande mwingine, migogoro inayoendelea sasa inadaiwa kuibuliwa na hatua ya uongozi kufuta uchaguzi wa rais wa Daruso kwa madaai kuwa hizo ni njama za kutaka mgombea anayeungwa mkono ya uongozi wa chuo ndiye ashinde.

Wakati hali hiyo ikitokea, mgombea mmoja, ambaye ni raia wa Uganda, Odong’ Odwar, alizuiwa kuwania nafasi hioyo kwa madai kuwa hajawasilisha vyetu vyake vya elimu. Uchaguzi huo umepangwa kufanyika kesho na jina la mgombea huyo halimo miongoni mwa wagombea.

Baada ya uchaguzi huo kumamishwa wanafunzi watano waliokuwa karibu na mgombea huyo walifukuzwa chuo kwa madai kuwa walikuwa wanavunja taratibu za chuo, ili kumvunja nguvu Odwar na baadaye alisimamishwa masomo kwa maelezo kuwa, kuna angalizo lilitolewa kwa utawala kuhakiki uhalali wake wa kuwepo chuoni hapo, pamoja na kupeleka nyaraka za matokeo (result slip)

Licha ya kupeleka nyaraka hizo uongozi huo ulidai cheti halisi na baada ya hilo kutokea, Odwar aliomba kwa baraza la mtihani la Uganda kuandika barua inayoeleza kuwa bado vyeti hivyo havijatolewa, jambo ambalo uongozi wa UDSM umelikataa.

Pia wanafunzi hao wanadai baada ya utawala kusimamisha uchaguzi huo, ili azma yao itimie waliamua kuwashawishi wajumbe wa bodi ya Rufaa ya Uchaguzi kujiuzulu ili kiwe kama kisingizio cha kuendelea kukwamisha uchaguzi huo na baada ya kugundua kuwa Waziri Mkuu wa Daruso, Julias Mtatiro ana mpango wa kutumia Bunge la chuo kuhoji walimsimamisha kusimamishwa kwa uchaguzi huo.

No comments: