Friday, April 25, 2008

Mkapa achunguzwa

SERIKALI imesema kuwa imeshaanza kufuatilia taarifa za tuhuma kuhusu matumizi mabaya ya madaraka dhidi ya viongozi wa serikali ya awamu ya tatu na iwapo itathibitika walitenda makosa watawachukuliwa hatua zinazostahili.

Kauli hiyo ilitolewa Bungeni jana na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, wakati alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF), aliyetaka kujua serikali inawashughulikia vipi viongozi wa serikali ya awamu ya tatu, wakiongozwa na rais smataafu Benjamin Mkapa, wanaodaiwa kutumia ofisi za umma kwa maslahi binafsi.

Hii ni mara ya kwanza kwa serikali kueleza kuwa inawachunguza watendaji wake wa serikali iliyopita na ni hatua tofauti na kauli iliyowahi kutolewa na rais Jakaya Kikwete, akitaka watu ‘wanaomfuatafuata’ rais Benjamin Mkapa wamwache apumzike.

Katika swali hilo la moja kwa moja, Hamad alisema baadhi ya viongozi chini ya rais Mkapa, walianzisha kampuni binafsi ilhali sheria ya maadili ya umma ya mwaka 1995 hairuhusu kiongozi kuitumia ofisi ya umma kwa maslahi binafsi au biashara.

Akijibu swali hilo, Pinda alisema serikali inazifuatilia taarifa hizo na kama ikijiridhisha na ukweli wa taarifa hizo, itachukua uamuzi ambao utakuwa na maslahi kwa taifa.

“Ni kweli hivi karibuni kumeibuka kwa tarifa hizo za viongozi kutumia ofisi za umma kwa maslahi binafsi, lakini kwa upande wetu ni lazima tujiridhishe, ili tutakapoamua tuamue kwa maslahi ya taifa,” alisema Pinda.

Aidha, katika swali la nyongeza, Hamad alitaka kujua ni kwa nini serikali inatumia muda mrefu kutoa uamuzi wa jambo hilo, wakati Wakala wa Usali wa Biashara na Makampuni (BRELA) wanazo taarifa za viongozi hao kufungua kampuni ya kibiashara.

Aidha, alihoji ni kwa nini wahalifu wengine wanafikishwa mahakamani haraka na hukumu zao kutolewa, lakini kwa viongozi hao mambo yao yanachelewa.

“Mimi sioni ni kwa nini serikali haitoi uamuzi mara moja wakati jambo liko wazi na hata BRELA wana taarifa za viongozi hao, na kwa nini hawapelekwi mahakamani?” alihoji Hamad.

Akijibu swali hilo, Pinda alisema ni lazima watu watofautishe sheria ya maadili ya viongozi wa umma na sheria ya makosa ya jinai.

Alisema ni vigumu kuwapeleka viongozi hao mahakamani kwani bado hawajawa na ushahidi wa kutosha kujua kama kosa lilofanywa ni la jinai au la maadili ya umma.

Alisema makosa ya maadili ya umma ni lazima kwanza wayaangalie kisiasa na kama yatathibitika kuwa ni ya jinai ndipo humpeleka mtu mahakamani.

“Suala la kumpeleka mtu mahakamani ni jambo kubwa sana na kabla ya kufanya hivyo ni lazima ujue kosa alilofanya ni la jinai au la kukiuka maadili ya umma, lakini kama tutajiridhisha na kile kilichofanyika ni jinai basi tutapeleka kunakohusika,” alisema Pinda.

Majibu hayo ya Serikali ni yametafsiriwa na baadhi ya wabunge kuwa ni ishara ya kuelekea kuchukuliwa hatua dhidi ya viongozi wa serikali ambao katika siku za hivi karibuni wamekuwa wakitumia ofisi za umma kwa maslahi binafsi.

Miongoni mwa mambo ambayo Mkapa na aliyekuwa Waziri wake Daniel Yona, wanahusishwa nayo ni kumiliki kampuni ya kuzalisha umeme ya Tanpower Resources Ltd.

Kampuni hiyo inahusishwa na mkataba wa kujiuzia mradi wa makaa ya mawe wa Kiwira mkoani Mbeya kwa bei ya kutupa ya sh milioni 700 na katika mazingira yanayozua maswali mengi hadi hivi sasa, walilipa sh milioni 70 tu na kukabidhiwa mradi huo ambao inaelezwa kuwa thamani yake inazidi sh bilioni 4.

Aidha, kampuni hiyo iliingia mkataba wa kuiuzia umeme Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) ambao itakuwa ikijipatia sh milioni 146 kila siku.

Hii ni mara ya pili kwa tuhuma dhidi ya Rais Mkapa na viongozi wake kutajwa bungeni baada ya juzi Mbunge wa Vunjo, Aloyce Kimaro (CCM), kuwatuhumu viongozi hao kumiliki kampuni ya uzalishaji umeme kinyume na taratibu za maadili ya umma.

Aidha, mbunge huyo alisema huo ni mfano mbaya zaidi kwa taifa hasa kwa mawaziri vijana wanaopewa nafasi ya kuziongoza Wizara nyeti.

2 comments:

Simon Kitururu said...

Isije ikawa ni uchunguzi wa maneno tu na sio vitendo:-(

Unknown said...

Nasikia wa Mramba umeshakamilika, karibu atafikishwa mahakamani