Monday, April 21, 2008

Kwa kuwa Serikali imezidiwa…

Nilikuwepo katika hoteli ya Movenpick wakati Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Said Mwema alipowaambia wahariri wa habari kuwa mafisadi wa EPA (akimaanisha watu wanaotuhumiwa kuiba fedha za umma kupitia akaunti ya malipo ya madeni ya nje iliyoko Benki Kuu), ni sawa na magaidi ambao wameiteka ndege.

Mwema alitoa mfano huu kutaka kuwaaminisha wahariri hao kwa nini timu ambayo yeye ni mjumbe wake, inayochunguza wizi huo, inashindwa, si tu kuyataja majina ya watuhumiwa ambao tayari wameshaanza kurejesha fedha walizoiba, bali pia kuwachukulia hatua za kisheria wakati huu.

Akitetea hatua zinazochukuliwa na timu hiyo inayoongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Johnson Mwanyika, na kumhusisha Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Edward Hosea, kama mjumbe wa tatu, Mwema alisema kuwa iwapo timu yake haitokuwa makini, wezi wa fedha za EPA wanaweza kutenda kama magaidi ambao wanaweza kuilipua ndege waliyoiteka ikiwa na mateka wake ndani.

Nikiri kuwa wakati niliposikia kauli hiyo ya Mwema kwa mara ya kwanza pale Movenpick, sikuona mara moja ukubwa wake. Ilikuwa mkapa siku ya pili, nilipoitafakari wka kina ndipo nilipobaini kuwa kuna uwezekano Mwema, labda kwa lengo la kutaka kujikosha kuwa anachokifanya kipo juu ya uwezo wake, aliamua kuonyesha kimafumbo ni jinsi gani mafisadi wameikamata serikali.

Kwa vyovyote vile, katika hali ya kawaida, haiwezekani kwa vyombo vikubwa vilivyokabidhiwa dhamana ya kutunza sheria katika nchi kama vile ofisi ya Mwanasheria Mkuu, Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), wapate ushahidi dhahiri dhidi ya wezi, halafu washindwe kuwachukulia hatua.

Na hivi ndivyo ilivyotokea kwa uchunguzi unaofanywa na vyombo hivi ndivyo ilivyotokea kwani timu hii baada ya kuwahoji wezi hao, ilipata ushahidi wa dhahiri kiasi kwamba baada ya mashauriano, wezi waliona kuwa hakuna njia nyingine ya kukataa kosa hilo na wakaamua kuanza kurejesha fedha hizo.

Kwamba wamekubali kurejesha ni uthibitisho wa wazi kuwa waliiba, na ndio maana nimeamua bila kumung’unya maneno kwuaita wezi. Kwamba fedha hizo ziliibwa ilishathibitishwa na Ernst & Young katika ukaguzi uliogfanyika na hata rais Jakaya Kikwete alishawishika na kuyakubali matokeo ya uchunguzi huo kiasi cha kufikia uamuzi wa kumfuta kazi aliyekuwa gavana wa Benki Kuu, Daudi Ballali.

Katika mazingira ambayo wezi wameamua kurejesha fedha walizoiba, mwendesha mashitaka anahitaaji ushahidi gani mwingine ili kujihakikishia ushindi katika kesi yake? Ni dhahiri kuwa mwendesha mashitaka anapoeleza kuwa haweza hata kuyataja majina ya wezi hao, kuna nguvu za ajabu nyuma ya woga huo.

Kwa kuwa timu hii ilipewa kazi na Rais, ninashawishika kuamini kuwa rais hawezi tena kuwageuka na kuwatisha ili wasifanye kazi yao ipasavyo. Hivyo, ni dhahiri kuwa nguvu hii haitoki katika mamlaka mahsusi zilizopo na hapa ndipo kauli ya Mwema akiwafananisha wezi hawa na magaidi walioteka ndege ilipoanza kunikolea na kupata maana halisi.

Ndio maana sasa ninaamini kuwa serikali imezidiwa na mafisadi katika hili la EPA. Na kwa kuwa serikali imezidiwa na mafisadi, ningependa kuchukua nafasi hii kuwashauri watanzania wenzangu kuwa umefika wakati sasa wa wananchi sisiw a kawaida, kuisaidia serikali katika kupambana na mafisadi. Nashauri tuangalie namna ya kutumia nguvu ya umma ili mafisadi wasiilipue serikali yetu na sisi tukiwa ndani yake, kama ambavyo magaidi wanavyoweza kuilipua ndege na mateka wake.

Awali, kabla hatujalishuhudia hili la EPA, Rais Kikwete alipochagua Baraza jipya la Mawaziri mwezi wa pili, watu wengi waliulalamikia uteuzi wa Andrew Chenge, wakimtuhumu kuwa ni mmoja wa mafisadi. Tuhuma hizi zilimfikia mwenyewe Chenge na alipotakiwa aeleze ni kwa nini, licha ya tuhuma hizo zote, ameteuliwa, yeye aliwaambia wanaohoji hilo waende wakamuulize rais ambaye ndiye aliyemteua.

Mimi nilikuwa ni mmoja wa watu ambao nilimuuliza Chenge hilo na siku ambayo Baraza hilo liliapishwa pale Chamwino, Dodoma. Mara aliponijbu hivyo, nilijaribu kumsogelea rais Kikwete kwa lengo la kulipenyeza swali hilo kutokana na ushauri wa Chenge. Rais alikuwa amezungukwa na watu wengi na alipotuona waandishi tukimnyemelea, alituwahi na kutueleza kuwa asingeweza kusema lolote kwa wakati huo kwa sababu alikuwa ameshasema sana, na kuwa atasema tena siku hiyo jioni kwenye hafla iliyokuwa imeandaliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Nilitarajia kuwa rais angelizungumzia hilo katika hotuba yake jioni hiyo, lakini hakuligusia. Labda alikuwa hajui kuwa tulitaka kumuuliza hilo. Lakini siku zilizofuata, bila shaka alisoma kwenye vyombo vya habari kuhusu tuhuma dhidi ya Chenge na lawama kwake kwa nini aliamua kumteua kuwa waziri. Kwa badati mbaya sana, hadi leo rais hajajibu hilo, licha ya kupata fursa kadhaa za kuzungumza na wananchi.

Sasa kama miujiza vile, habari zinapatikana kuwa kilichokuwa kinadhaniwa kuwa ni tuhuma tu, kinaweza kuwa ni habari ya uhakika; Chenge ni bilionea. Katika hili tatizo si ubilionea wak, bali ameupataje ubilionea huo wakati akiwa mtumishi wa serikali hii ambauyo inanuka umasikini kushoto kulia, mbele nyuma, juu na chini?

Haiyumkini kuwa Rais Kikwete hakuwa na chaguo jingine badala ya Chenge. Nini kimemsukuma kuchagua mtu ambaye uadilifu wake una mashaka, kinaweza kuwa ni nguvu zile zile zilizotajwa na Mwema.

Ninachokihisi hapa ni kuwa kuna uwezekano kuwa rais naye amezidiwa katika hili na ndio maana narejea ushauri wangu kwa watanzania wenzangu kuwa imefika wakati sasa wananchi tujitoe muhanga kumsaidia rais kupambana na nguvu hizi. Naamini kuwa nguvu za umma hazitashindwa.

Uundwaji wa baraza hilo la mawaziri ulitokana nay ale yaliyoibuka baada ya kuwasilishwa bungeni kwa ripoti ya Kamati teule ya Bunge kuhusu mradi wa kuzalisha umeme wa harura uliotolewa kwa kampuni ya Richmond ya Marekani. Aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowasdsa akajiuzulu na Baraza la Mawaziri likavunjika.

Lakini inaonekana kuwa hichio kilikuwa ni kisa tu na sasa mkasa wenyewe unaonekana huko huko bungeni kupitia Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz. Wakati ripoti hiyo ilipowasilishwa na aliyekuwa mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk. Harrison Mwakyembe, ilijadiliwa kwa jazba sana. Katika mchango wake wa maandishi, Aziz alituhumu kuwa kamati ilikiuka misingi ya kuundwa kwake kwa kufanya kazi nje ya muda iliyopangiwa, na hivyo kufanikisha kuandaa ripoti mbili, ikiwamo moja ambayo ni bandia (fake).

Hizi ni tuhuma nzito sana na mara moja zilipata mshtuko wa Bunge kama taasisi na kamati kama chombo kilichotekeleza azimio la bunge. Kutokana na hilo, Bunge, kupit6ia tangazo lililotolewa na Spika, Samwel Sitta, lilimtaka Aziz, kuthibitisha kile alichokisema, kama inavyotakiwa katika moja ya kanuni za Bunge zinazokataza Mbunge kusema uongo Bungeni.

Aziz alitakiwa kuthibitisha ukweli ya aliyoyaeleza kwa kuwasilisha maelezo kuhusiana na kauli yake hiyo. Kwa kuwa muda wa mkutano uliojadili masuala hayo ulikuwa umemalizika, Aziz alitakiwa kufanya hivyo katika mkutabno uliofuata.

Lakini tumeshuhudia maajabu kwani Soika huyo huyo, ambaye ndiye aliyetangaza kuwa Aziz anatakiwa kujieleza kwa mujibu wa kanuni, leo hii ameyazuia maelezo ya Mbunge huyo kwa maelezo kuwa kuyawasilisha Bungeni ni kukiuka kanuni kwa sababu kamati inayotuhumiwa ilishamaliza kazi yake kwa hiyo haiwezi kujitetea.

Kinachoshangaza ni kwua wakati uamuazi wa kumtaka Aziz ajieleza ulitolewa na Bunge, uamuazi wa kuyakataa maelezo yake wala haukulihusisha Bunge! Kilikuwa ni kikao cha viongozi wa CCM! Na kwa maneno yake mwenyewe, Aziz amesema kuwa amekubaliana na hoja ya kumzuia kusema Bungeni kutokana na kulinda maslahi ya chama chake.

Haya ni maajabu yaliyoje! Maamuzi ya Bunge yakaamriwe na kikao cha viongozi wa CCM! Hatua hiyo inanilazimisha nijiulize hivi Bunge lina uhusiano gani na CCM kiasi kwamba sehemu ya maamuzi yake yakafanywe na viongozi wa chama hicho? Ndio utaratibu tuliojiwekea huo?

Namshanga pia Spika kwa kusema sasa hivi kuwa Aziz kwuasilisha maelezo yake ni kukiuka kanuni wakati alipoamriwa akalete maelezo zilitumika kanuni hizo hizo. Kwani wakati huo hawakujua kuwa kamati hiyo ilikuwa imemailiza muda wake?

Pia, mapendekezo ya kamati hiyo yalifikishwa serikalini kupitia azimio la Bunge. Serikali ikasema kuwa inakwenda kuyafanyia kazi na itakuja kutoa maelezo yake Bungeni. Hili tunalisubiri. Ninachojiuliza ni kuwa iwapo katika maelezo yake, serikali itaituhumu kamati hiyo kwa jambo lolote, itakuwaje?

Najiuliza swali jingine; hivi itakuwa iwapo mmoja wa wabunge ataamua kuhoji kulikoni, mbona Aziz hajawasilisha maelezo yake kama ilivyokuwa imeagizwa na bunge atyajibiwa nini? Kwamba eti vkikao cha viongozi wa CCM kimeona ni ukiukwaji wa kanuni za bunge kumruhusu alete maelezo yake?

Mlolongo wa maswali haya ambayo kukosekana kwa majibu yake ya uhakika kunazua utata kunaonyesha kuwa si bure, lazima kuna nguvu nyingine ambayo zimesababisha kupindishwa kwa hoja ya Aziz na kuondolewa Bungeni kinyemela hadi kwenye vikao vya viongozi wa CCM ambao walijipa nguvu ya kuamua hoja iliyotolewa Bungeni.

Inaonekana wazi kuwa Bunge limezidiwa na nguvu fulani kiasi kwamba limekubali kupokonywa hoja hii na CCM. Na ndio maana sitachoka kuwaomba watanzania wenzangu kuwa nao wasichoke, tujitolee kulipigania Bunge letu.

Naamini kuwa kwa umoja wetu, tunaweza kuuondoa unyonge tulio nao na kupata nguvu ya kulisaidia Bunge kupambana na nguvu hizi zisizoonekana. Na hapa naomba tuitumie nguvu ya umma kulikomboa Bunge letu.

Kwa ujumla wake, serikali inaonekana kushikwa na kigugumizi tangu tuhuma za ufisadi dhidi ya watumishi wake na wafanyabishara wakubwa, zianze kutajwa hadharani. Tangu wakati huo, serikali haijafanya lolote lililoonekana dhahiri, kuwa ni juhudi zake za kupambana na ufisadi.

Baadhi ya waliokuwa wametajwa katika orodha ya mafisadi na Dk. Wilbrod Slaa, walitishia kwenda mahakamani kwa madai kuwa wamekashifiwa. Hiyo ilikuwa ni hatua nzuri ambayo ingesaidia kuwasafisha lakini kwa mshangao wa wengi, hadi hii leo wameshindwa kufanya hivyo.

Kushindwa kwao ni moja ya dalili kuwa huenda kilichoelezwa na Dk. Slaa ni kweli, na kuwa iwapo mamlaka zinazohusika zingetaka kulishikia bango suala hilo, hapo palikuwa mahali pazuri pa kuanzia. Lakini hadi leo, si jeshi la Polisi, Takukuru wala taasisi nyingine yoyote inayohusika na vita dhidi ya ufisadi ambayo imeonekana kuzifanyia kazi tuhuma zilizotolewa na Dk. Slaa ambazo wahusika wameshindwa kuzikanusha.

Kwa ujumla inaonekana kuwa serikali na taasisi zake zinakwazwa na nguvu fulani ambayo haionekani wazi. Na ndio maana narudia tena kuutaka umma wa watanzania, tujifunge vibwebwe kwa ajili ya kuitetea serikali yetu dhidi ya nguvu hii kubwa ambayo tayari imeshajionyesha dhahiri. Naamini kwua katika umoja wetu tutashinda na kurudisha heshima ya serikali na nchi yetu.

Mungu na atubariki katika haralati hizo.

No comments: