Saturday, July 19, 2008

Dk. Migiro yupo likizo Dar

NAIBU Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Dk. Asha Rose Migiro, yupo nchini kwa ajili ya likizo. Akizungumza leo, ameisifu Tanzania kwa jitihada za kukuza elimu na kupunguza vifo vya akina mama na watoto.

Amesema sifa hizo kwa Tanzania zinatokana na mafanikio hayo ambayo yanaendana na utekelezaji wa Malengo ya Milenia ya Umoja wa Mataifa, yanayopaswa kufikiwa ifikapo mwaka 2015.

Amesema hatua zinazochukuliwa na Tanzania katika kukabiliana na umaskini ni za kujivunia na za kuigwa.

Dk. Migiro, ambaye yuko nchini kwa likizo yake ya kwanza tangu alipoteuliwa kushika wadhifa huo mwaka jana, alieleza kuwa ongezeko la uandikishaji wa wanafunzi nchini, uboreshaji wa huduma za afya ambazo zimepunguza idadi ya vifo vya akina mama na watoto pamoja na usawa wa kijinsia ni maeneo ya msingi ambayo Tanzania imefanya vizuri kuliko mataifa mengine ya Afrika.

Kuhusu upatikanaji wa ajira katika Umoja wa Mataifa, alisema habari kwamba Watanzania wananyimwa fursa za ajira katika Umoja huo kulinganisha na wenzao wa Kenya, Uganda na nchi za Afrika Magharibi si za kweli kwa vile unatoa fursa sawa kwa wote wanaotimiza vigezo ikiwamo kufaulu mitihani inayotolewa.

Aliwahamasisha vijana wa kitanzania kusoma lugha zaidi ya moja zinazotumiwa na umoja huo kwa sababu kujua Kiingereza pekee si kugezo kinachotosha kupata ajira katika umoja huo.

Dk. Migiro ambaye ni Mwanamke Mwafrika wa Kwanza duniani kuteuliwa katika wadhifa huo, yupo nchini kwa likizo yake ya kwanza na anatarajiwa kukutana na Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Rais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Aman Abeid Karume.

No comments: