Thursday, November 13, 2008

NEWS UPDATE: DUCE nacho chafungwa

Habari zilizopatikana mchana huu zimethibitisha kuwa Chuo Kishiriki cha Chuo Kikuu cha dar es Salaam cha Ualimu (DUCE) nacho kimefungwa kwa muda usiojulikana.
hatua hiyo imekuja siku moja tu baada ya kufungwa kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kutokana na mgomo wa anafunzi.
Habari kutoka katika chuo hicho kilichop maeneo ya Chang'ombe jijini Dar es Salaam, zinaeleza kuwa uongozi wa chuo ulitoa trangazo la kukifunga chuo hicho leo asubuhi, wakati wanafunzi wanaingia katika siku ya pili ya mgomo wao.
Tangazo hilo liliwataka wanafunzi kuwa wameshaondoka chuoni hapo ifikapo saa 7 mchana. Tayari magari ya askari Polisi wa doria na wale wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia, yalionekana katika maeneo ya chuo hicho, wakati wanafunzi wakifungasha mizigo yao tayari kwa kuondoka.
Hata hivyo, wanafunzi hao walisema kuwa kufunga chuo si suluhisho la tatizo hilo kwani watakaporudishwa chuoni hapo wataendelea na mgomo wao hadi wapate haki yao.
Taarifa zaidi kutoka Morogoro zinaeleza pia kuwa wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) nao wanapanga kugoma kuwaunga mkono wenzao wa UDSM.
Wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu nchini wapo katika mgogoro na serikali wakipinga sera ya uchangiaji wa elimu ya juu, wanayodai kuwa inawanyanyasa na kuwabagua watanzania kutokana na uwezo wao kiuchumi.
hata hivyo, serikali inaitetea sera hiyo, ikisema kuwa inawezesha kwuasaidia wanafunzi kulingana na uwezo wa wazazi wao.

No comments: