Tuesday, December 2, 2008

NEWS UPDATE: Mramba, Yona nje

Mawaziri wa Zamani, Basil Mramba na Daniel Yona, leo wameachiwa kwa dhamana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya kusota gerezani kwa muda wa wiki moja.
Vigogo hao walipata dhamana baada ya kukata rufaa Mahakama Kuu kupinga masharti magumu waliyowekewa na Mahakama ya Kisutu na jaji Njengafibili Mwaikugile alilegeza masharti hayo. Mahakama ya Kisutu iliwataka watuhumiwa hao kutoa dhamana ya fedha taslimu kiasi cha sh bil 3.9 kila mmoja.
Mahakama kuu ilibadili sharti hilo na kupunguza kiwango cha fedha hadi sh bil 2.9 na kuwaruhusu kuweka hati za mali zenye thamani kama hiyo.
Lakini Mahakama Kuu iliachia masharti mengine kama yalivyo. Nayo ni kuwasilisha pasi zao za kusafiria, kutotoka nje ya dar es Salaam bila idhini ya Mahakama na kuwa na wadhamini wawili wanaoaminika.
Mramba aliwasilisha hat tatu ambazo zilikuwa na thamani ya zaidi ya sh bil 3 zenye majina tofauti, hyuku moja tu ikiwa na jina lake. Yona aliwasilisha hati tatu za thamani ya zaidi ya sh bil 3 zote zikiwa na majina yake.
Katika serikali ya awamu ya Tatu, Mramba alikuwa waziri wa fedha na Yona waziri wa Nishati na Madini. Wanatuhumiwa kutumia madaraka yao vibaya wakiwa mawaziri kwa kuingia mkataba ya kampuni ya ukaguzi wa dhahabu ya Alez Sterwat kinyume na sheria ya manunuzi na kuisababishia serikali hasara ya sh bil 11.7

No comments: