Tuesday, January 29, 2008

Wabunge Wadai Ripoti Kamili ya Ernst & Young

SASA inaelekea mambo yataanza kunoga. Wabunge wameshaanza kuidai ripoti kamili iliyoandikwa na kampuni ya Ernst & Young kuhusiana na ubadhirifu uliobainika katika Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), iliyopo Benki Kuu (BoT).

Wabunge walitoa msimamo wao huo jana, mara baada ya Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, kumaliza kuwasilisha bungeni kauli ya serikali ambayo ilikuwa ni taarifa kuhusu ripoto ya ukaguzi wa EPA.

Wabunge waliona huo ni mwanzo wa ubabaishaji kwani alichokiwasilisha Meghji ilikuwa ni muhtasari wa kilichomo katika ripoti ya Ernst & Young, na hatua ambazo rais Jakaya Kikwete na Wizara yake imezichukua baada ya kukabidhiwa ripoti hiyo.

Taarifa hiyo ya Meghji, haina tofauti sana na taarifa ambayo ilitolewa kwa vyombo vya habari na Katibu Mkuu Kiongozi, Phillemon Luhanjo, ikielezea kilichobainika katika ukaguzi uliofanywa na Ernst & Young na hatua ambazo rais Kikwete alizichukua.

Baada ya kumaliza kusoma kauli hiyo, Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP) na Christopher ole Sendeka (Simanjiro-CCM), walisimama wakitaka mwongozi wa Spika kuhusiana na suala hilo.

Alipopewa nafasi ya kusema, Cheyo alieleza kuwa taarifa iliyoeasilishwa na Meghji ni nzuri, lakini akabainisha kuwa ni finyu mno ukilinganisha ya ripoti ya Ernst & Young.

Aidha, Cheyo alihoji iwapo ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) itawasilishwa Bungeni na kutaka tipoti hiyo, pamoja na taarifa ya Meghji, vyote vijadiliwe na wabunge kwa kina

Kwa upande wake, Sendeka aliposimama, alibainisha kuwa kilichowasilishwa na Waziri Meghji ni muhtasari tu.

Huku akimwelekea Spika, ole Sendeka alisema: “Naomba kama itakubalika uielekeze serikali ilete taarifa kamili ya mkaguzi (Ernst & Young) na bunge lipate fursa ya kuijadili kwa kina.”

Kwa kuoinyesha kuwa wanaunga mkono yanayowasilishwa na wenzao, wabunge wengi walikuwa wakishangilia kwa kupiga makofi wakati wabunge hao wawili walipokuwa wakiwasilisha hoja zao.

Akijibu maombi hayo, Spika Samuel Sitta alikubaliana na hoja za wabunge hao na kusema kuwa yote waliyaomba yamo katika mchakato wa mashauriano baina ya ofisi ya Spika na serikali.

Aliwakumbusha watoa hoja na wabunge wengine kwua tangu awali, alishakubaliana na hoja iliyowasilishwa na Lucy Mayenga (Viti Maalum-CCM), akitaka ripoti ya hesabu za BoT za mwaka 2005/06 iwasilishwe bungeni na kujadiliwa na wabunge wote.

“Hoja hii bado ni hai na taarifa iliyotolewa leo si kipingamizi. Naamini kuwa katika wakati huu wa uwazi na ukweli serikali imeeshasikia hoja zenu na itazitafakari ipasavyo na bila shaka tutafikia mahali pazuri,” alisema Spika Sitta.

Katika taarifa aliyoiwasilisha jana Bungeni, pamoja na kubainisha yaliyogunduliwa na Ernst & Young katika ukaguzi wa EPA na hatua zilizochukuliwa na rais, meghji alisema kuwa wizara yake nayo imechukua hatua kadhaa.

Alisema kuwa baada ya kupata ripoti hiyo, Wizara ya fedha imeiagiza Mamlaka ya Mapato cnhini (TRA), kufanya uchunguzi wa kina kubaini mienendo ya ulipaji kodi wa makampuni yote yaliyohiska katia kashfa ya EPA.

Aidha, Meghji alisema kuwa iwapo itabainika kuwaepo kwa ukwepaji wa kodi, TRA imetakiwa kuchukua hatua za kisheria.

Pia wizara yake imeielekeza BoT kufanya uhcunguzi wa kina na kuwasilisha taarifa serikalini kuhusu hatua zilizochukuliwa kwa mabenkiya biashara yaliyohusika na kupokea fedha kutoka makampuni yaliyotajwa kuhusika katika kashfa ya EPA, iwapo sheria, taratibu na kanuni kuhusu udhibioti wa fedha haramu zilizingatiwa.

Aidha, akifafanua hatua ya rais Kikwete kuwaagiza Mwanasheria Mkuu wa serikali (AG), Mkurugenzi wa Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP) kuchunguza zaidi suala hilo, unalenga kupata ushahidi wa kisheria utakaowezesha kufunguliwa kwa mashtaka dhidi ya watu na kampuni zote zilizohusika katika kashfa ya EPA.

Thursday, January 17, 2008

Mgonja Anangoja Nini Hazina?

HATUA ya Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa Daudi Ballali kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) inadhihirisha kuwa kulikuwa na makosa makubwa katika taasisi hiyo nyeti. Ukubwa wa makosa hayo unaweza kuonekana kupitia hatua hiyo ya rais ambayo kwa namna yoyote ile ni hatua kubwa mno.
Hatua yake ya kuagiza vyombo kadhaa kufanya uchunguzi na kuwachukulia hatua watu wengine waliohusika na kashfa hiyo, inadhihirisha pia kuwa Ballali si mhusika pekee katika sakata hili. Wapo wengine wengi tu ambao baadhi yao ni rahisi kuwatambua kutokana na nafasi zao.

Mtu asiyeweza kukwepa kunukia tuhuma hizi moja kwa moja ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha. Kwa mujibu wa wadhifa huo, mtu huyo ndiye anayehusika kuidhinisha malipo ambayo serikali inayafanya. Kwa Kiingereza yeye anaitwa ‘Paymaster General.’

Kashfa iliyomng’oa Ballali inahusiana na malipo. Ni malipo ya Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) iliyopo BoT. Kwa sababu malipo haya yalifanywa na serikali ni dhahiri kuwa ‘Paymaster General’ aliidhinisha yafanyike.

Malipo yaliyotiliwa shaka na kuchunguzwa ni yale yaliyofanyika kipindi cha 2005/2006 wakati huo Gray Mgonja akiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha pamoja na Peniel Lyimo. Lyimo alikwishaondolewa wizarani hapo lakini Mgonja bado anaendelea na wadhifa wake huo hadi hivi sasa.

Iwapo tunataka kupata maelezo ya kina kuhusiana na malipo haya, Mgonja na Lyimo wanaweza kutusaidia sana. Watatusaidia kwa sababu wao au mmoja wao - kulingana na mgawanyo wa kazi zao - ndio walioidhinisha malipo haya.

Kwa kawaida ‘paymaster general’ anaidhinisha malipo baada ya kujiridhisha kuwa malipo hayo ni halali na yanatolewa kwa kufuata taratibu zote za kiserikali zilizopo. Itashangaza sana iwapo ‘paymaster general’ akaamua kutoa tu fedha na kuzilipa bila kufuata taratibu hizo.

Kwa maana hiyo, Mgonja na Lyimo wanayo nafasi nzuri ya kutueleza Watanzania nini hasa kilifanyika katika malipo haya. Wala wasikwepe hili kwa namna yoyote ile kwa sababu wao ndio walihusika kuidhinisha malipo hayo.

Watueleze ilikuwaje wakakubali kuidhinisha malipo ya mabilioni haya ya fedha za wavuja jasho na kututia hasara kiasi hicho? Umakini wao uko wapi katika kuidhinisha malipo ya fedha zetu? Iwapo waliweza kuidhinisha malipo haya yenye kutia shaka, watashindwaje kuidhinisha malipo mengine mengi tu tusokuwa na habari nayo?

Uchunguzi uliofanywa unahusu mwaka 2005/2006 lakini akaunti ya EPA imefanya kazi kwa miaka mingi na Mgonja na Lyimo (pamoja na wengine) wamekuwapo wizarani wakiidhinisha malipo kupitia akaunti hii kwa miaka hiyo yote.

Inashangaza kuwa Mgonja bado anaendelea kuwapo madarakani hadi hivi sasa, wakati kasoro kubwa kama hii imeshajitokeza na Rais ameshawaonyesha Watanzania kuwa kuna kasoro kubwa kiasi cha yeye kutengua uteuzi wa gavana.

Kuna uwezekano kuwa gavana alihusika na wizi uliogunduliwa lakini pia kuna uwezekano kuwa hakuhusika. Kama alihusika hiyo ni sababu tosha ya Rais kusikiliza na kutekeleza maombi ya watu wanaotaka Ballali arudi nchini kuja kukabili mashtaka kuhusiana na kadhfa hiyo ya EPA.

Lakini kama hakuhusika, alipaswa kuwajibika kwa sababu yeye kama kiongozi wa taasisi nyeti, alipaswa kubaini ujanja huo uliofanywa na watu wengine na kuuzuia.

Ndiyo maana tulimwamini kuwa gGavana wa BoT. Hata kama hakuhusika, kutokea kwa wizi huu kunamaanisha kuwa Ballali hakuifanya kazi yake ipasavyo. Na ndiyo maana Rais hakuona kigugumizi na kuchukua hatua ya kutengua uteuzi wake mara moja.

Sasa ndugu yetu Mgonja, wewe ndiye uliyeidhinisha malipo ya mabilioni hayo yote; hivi hauoni tu kuwa nawe unahusika kwa karibu mno na kashfa hii? Au unataka hadi Rais atengue uteuzi wako pia? Hata kama hukuhusika, kwa nini usiwe mstaarabu na kuamua kuachia ngazi ili ule uchunguzi aliosema rais ufanyike uje ukusafishe?

Mgonja anatakiwa kutambua kuwa watu wanaomwangalia na kumpima katika hili, wanarejea tuhuma nyingine alizowahi kutupiwa huko nyuma naye akashindwa kuzitolea majibu ya kuridhisha.

Watu bado wanakumbuka kuwa jina lako lilikuwamo kwenye orodha ya viongozi waliotuhumiwa kwa ufisadi. Wewe mwenyewe ulikaririwa kuwa utashitaki kwa sababu umepakaziwa. Lakini hadi leo haijajulikana kesi yako imekwama wapi!

Hilo lina tafsiri kubwa sana machoni pa Watanzania na sasa inapobainika kuwa ulikuwapo katika Wizara ya Fedha kama ‘paymaster general’ wakati malipo ya EPA yanafanyika mwaka 2005/2006, Watanzania wamepata kitu kingine cha kukupima.

Hata kama ulitumiwa kuidhinisha malipo hayo bila ya wewe mwenyewe kujua, unatakiwa kuwajibika kwa sababu utakuwa ulishindwa kufanya kazi yako vema na kubaini kuwa malipo hayo yalikuwa na mushkeli.

Ningependa kukushauri kuwa uwe muungwana na ujiondoe haraka iwezekanavyo kwa sababu hata ufanye nini, utaendelea kunukia marashi ya EPA. Hilo hauwezi kulikwepa.

Wednesday, January 16, 2008

BREAKING NEWS- Balali anyang'anywa Visa na Marekani

Habari za uhakika nilizozipata hivi punde zinaeleza kuwa aliyekuwa Gavana wa BoT, Daudi ballali, amenyang'anywa visa na serikali ya Marekani.
taarifa hizo zinaeleza kuwa Marekani imefikia uamuzi huo baada ya kuthibitishiwa na serikali ya Tanzania kuwa Ballali si mwakilishi tena wa serikali.
Marekani tayari imeshaitaarifu serikali ya Tanzania kuwa inabatilisha viza ya Balali kwa sababu haiwakilishi tena Tanzania.
Kwa mujibu wa vyanzo vyangu, Balali alipewa viza hiyo kutokana na wadhifa wake kama Gavana, akiiwakilisha Tanzania katika nchi mbalibali ikiwamo Marekani.
Lakini kwa sababu ajira yake imekoma, Marekani imeona kuwa hana sifa za kuwa na visa hiyo ambayo inaitwa kwa kimombo non-immigrant visa.

Dk. Willbrod Slaa; Muasisi wa hoja ya Ufisadi iliyomng'oa Ballali

KATI ya watu waliotakiwa wawe na furaha baada ya Rais Jakaya Kikwete kutangaza kutengua uteuzi wa aliyekuwa gavana wa Benki Kuu (BoT), Dk. Daudi Ballali, ni Dk. Wilbrod Slaa, Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na Mbunge wa Karatu.
Lakini hali si hivyo kwa Dk Slaa. Kilichofanywa na Rais Kikwete hakijamridhisha kiasi cha kutosha. Anaamini kuwa sehemu iliyoshughulikiwa ni ndogo sana.

Kwamba Rais ametangaza uamuzi aliochukua kutokana na sababu alizozitoa, lakini kilichoelezwa ni sehemu ndogo sana ya tatizo kubwa lililopo.

“Tumeikubali taarifa, tunafurahi kuwa baadhi ya hatua zimewekwa hadharani, lakini serikali haijawa wazi kwa kiwango yenyewe ilichoahidi.

“Tuliambiwa kuwa ripoti ya uchunguzi uliofanywa na kampuni ya Ernst & Young itawekwa hadharani yote. Lakini walichofanya ni kutoa taarifa iliyotokana na sehemu ya ripoti, hilo silo walilotuahidi,” hivyo ndivyo anavyoeleza Dk. Slaa kuhusu kutoridhishwa na uwazi wa serikali kuhusu ripoti ya uchunguzi wa Ernst & Young.

Kingine kinachomfanya Dk. Slaa asifurahie sana hatua ya Rais Kikwete ni kuwa hata hicho kilichoelezwa katika taarifa, hakijibu sehemu kubwa ya matatizo yeye na wapinzani wenzake waliyojaribu kuyaonyesha.

Kipimo chake katika hili ni majina ya kampuni zilizotajwa kuhusika na kashfa ya akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA). Wakati akitangaza kwa waandishi wa habari taarifa ya serikali na hatua Rais Jakaya alizozichukua baada ya kukasirishwa na kuhuzunishwa ripoti hiyo, Katibu Mkuu Kiongozi, Phillemon Luhanjo, aliyataja makampuni 22 kuwa yalihusika na malipo yenye kutia shaka ya EPA.

Lakini Dk. Slaa anasema kuwa hiki ni kiinimacho kwa sababu kampuni zilizotajwa zinahusisha watu wadogo sana na sehemu ndogo sana ya ubadhirifu ambao yeye ana taarifa nao.

“There is no way (haiwezekani), deep green isionekane humu, uchunguzi uliofanywa EPA unahusisha 2005/06. Mimi ninazo taarifa kuhusiana na nini kampuni hii imefanya, nina hadi cheque number (namba za hundi) zilizotumika kulipa mabilioni katika kampuni hii.
“Lakini inavyoonekana wao walichokitoa (katika taarifa ya Luhanjo) ni kile walichotaka kukitoa, kile ambacho kilistahili kutolewa kimefichwa “wamewataja watu wadogo sana,” anasema.

Katika sakata hili la ubadhirifu BoT na kashfa ya mafisadi, historia itaendelea kumuonyesha Dk. Slaa kama muasisi wa hoja hizo. Ingawa kabla yake kulikuwa na taarifa zilizosambaa chini chini kuhusiana na tuhuma za ufisadi na ubadhirifu, lakini yeye ndiye aliyeibua mambo hayo hadharani.

Aliposimama bungeni na kueleza mambo hayo, wapo waliomdhihaki wakidhani kuwa ulikuwa ni mchezo wa kisiasa uliozoeleka wa wapinzani kuwarushia makombora watu walio upande wa pili.

Lakini Dk. Slaa hakukatishwa tamaa na kejeli, dharau na masimango mengine yaliyotoka hata kwa viongozi wakuu serikalini (wako hata waliosema kelele za mlango hazimnyimi mwenye nyumba usingizi). Dk Slaa aliamua kusimama kidete akitetea hoja yake, akitumia taarifa alizozikusanya kutoka katika mtandao wa intaneti na vyanzo vingine.

“Ndiyo, nilitumia taarifa za kwenye intaneti kwa sababu nilijua kuwa zinaruhusiwa kisheria wakati (viongozi wa serikali) walipoleta sheria ya kutaka vyanzo vya intaneti vitumike kama ushahidi mimi nilipinga bungeni, lakini kutokana na wingi wao (wabunge wa CCM) waliipitisha, na nikaamua kuitumia hiyo hiyo,” anasema.

Utata kuhusu ushahidi wa Dk. Slaa uliotoka katika intaneti ulipingwa hata na Spika, Samuel Sitta, ambaye katika hatua fulani alionekana kuwa na shaka na ushahidi huo.

Lakini hii ni kama ilimchochea Dk. Slaa na kueleza nia yake ya kuandaa hoja binafsi, akilitaka Bunge liunde kamati teule kuchunguza tuhuma alizokuwa nazo.

Lakini Dk. Slaa hakufanikiwa kuiwasilisha hoja hiyo bungeni. Anaeleza sababu za kushindwa kuwasilisha hoja hiyo kuwa alipata taarifa mapema kuwa hoja hiyo ingezimwa.

“Sikutishwa na mtu. Nilipata taarifa kuwa hoja itazimwa, kulikuwa na tarifa zilizonifikia kuwa kiongozi mmoja serikalini alikuwa ametahadharishwa kuwa asije akaiacha hoja hii ikatua bungeni kwa sababu serikali haikuwa na majibu wakati ule.

“Walijiandaa kuikwamisha kwa namna yoyote na mimi nikaona kuwa iwapo nitaiwasilisha haitatendewa haki. Nikatafuta mahali muafaka pa kuipeleka na matokeo yake yameshaonekana,” anaeleza kwa kujiamini.

Maelezo haya ya Dk. Slaa yanamaanisha kuwa uamuzi wake pamoja na viongozi wenzake wa kambi ya upinzani kuichukua hoja hiyo na kuipeleka kwa wananchi, wakiifanya ajenda yao kuu katika mikutano ya hadhara iliyofanyika mikoa kadhaa nchini, ndiyo mahali muafaka alikoipeleka hoja hiyo.

Walianzia katika viwanja vya Mwembeyanga, Dar es Salaam, ambako Dk. Slaa alifanya kile ambacho watu wengi waliamini kuwa hakiwezi kufanywa na mwanasiasa wa Tanzania.

Siku hiyo, Dk. Slaa aliweka hadharani majina ya viongozi kadhaa wa serikali na chama, si tu akiwatuhumu kwa ufisadi, bali akiorodhesha tuhuma za kila mmoja wao.

Huko nyuma wanasiasa wa upinzani wamewahi kutaja majina mawili matatu ya watu wanaowatuhumu kwa ubadhirifu wa mali za umma lakini hoja hizo hazikupata mashiko.

Hii ya Dk. Slaa ilikuwa ni tofauti. Jitihada za watuhumiwa kutaka kujisafisha zilibakiwa kuwa matishio ambayo hayakumteteresha Dk. Slaa na wenzake.

Lakini Dk. Slaa alipata wapi ujasiri wote huu? Au ni namna nyingine ya kujitafutia umaarufu?

“Ndugu yangu, ukiyavulia nguo maji ya baridi huna budi kuyaoga. Mimi nilishayavulia nguo maji haya na hivyo nililazimika kuyaoga. Katika hili ninatimiza wajibu wangu kama mwakilishi wa wananchi, wala sitafuti jingine lolote, niliwaomba wananchi niwatumikie, wakanichagua na sasa natimiza ahadi ya kuwatumikia,” anasema.

Anaeleza zaidi kuwa ujasiri mwingine aliupata kutokana na kuwa na taarifa za uhakika kuhusu kile alichokisema.

Kwamba alikuwa na uhakika na taarifa alizokuwa nazo kwa sababu zilizotokana na taarifa za serikali yenyewe pamoja na vyanzo vingine. Dk. Slaa ni miongoni mwa wabunge na wanasiasa wenye tabia ya kusoma sana.

Yeye mwenyewe anaeleza kuwa hutumia muda wake mwingi kuperuzi habari mbalimbali kwenye intanet na ana muda maalumu wa kupitia rekodi za serikali na tafiti mbalimbali kuhusu masuala anayoyafuatilia.

Akisisitiza kuhusu usahihi wa taarifa alizo nazo kuhusu watu na makampuni anayoyatuhumu kwa ufisadi, anasema katika kutafuta taarifa za kampuni anazozituhumu, alifika ofisi za wakala wa kuandikisha kampuni (Brela) alikopata ushahidi wa yale aliyokuwa akiyafuatilia.

“Nilijifunza kufanya hivi baada ya sisi (wapinzani) kudharauliwa sana bungeni na kukejeliwa kuwa hatujui kufanya ‘research’ (utafiti) na sisi tukakiri kuwa kweli bado ni wachanga sana na tunajifunza, lakini katika uchanga wetu haya ndiyo tuliyoweza kuyafanya na bado tunaendelea,” anasema.

Anaeleza kuwa jambo lililomtia matumaini kuendelea na mapambano ya kuwataja hadharani watu waliojihusisha na ufisadi ni kilichotokea baada ya kutaja majina yao, ambapo walijitokeza Watanzania anaowaeleza kuwa wenye uchungu na nchi yao na ari ya kulitetea taifa lao, na kumpelekea taarifa nyingine nyingi za jinsi fedha za umma zinavyotafunwa na wachache.

“Hili ni kundi la Watanzania ambao wameanza kutuamini (wapinzani) kuwa tumedhamiria kupambana na maovu na ufisadi katika jamii,” anaongeza kuwa kati ya hao waliowasiliana naye ni watumishi kutoka serikalini, baadhi yao kutoka idara nyeti za serikali.

“Hawa si kwamba wametoa siri za serikali, kwa mujibu wa sheria namba 3 ya mwaka 1988 kifungu cha 10. Walichofanya ni kutoa taarifa za wizi na si siri za serikali, hivyo sheria hiyo haiwezi kutumika kuwabana.

“Ndiyo maana baada ya kupitia shida zote hizi na nyingine nyingi, sijaridhika na kilichotokea na kumweka nje Dk. Ballali. Wapo wengine wengi ambao nina ushahidi nao kuwa walihusika katika sakata hili, nao washughulikwe na kuwekwa pembeni.

“Hii si siasa, tunapigania maslahi ya nchi na ndiyo maana hata walipovamiwa wahariri wa ‘MwanaHalisi’ kila mtu alilaani, kwa sababu ule ulikuwa ni uvamizi dhidi ya demokrasia. Na ufisadi nao hivyo hivyo, hauna rangi ya chama cha siasa, unaumiza Watanzania wote na kuneemesha wachache.

“Tutaendelea kudai ripoti ya ukaguzi wa Ernst & Young iwekwe hadharani yote ili wananchi wajionee wenyewe kilichomo na hapo ndipo watakapogundua maana halisi ya kilichoonekana kuwa ni kelele za wapinzani.

“Sisi tunaonekana kama tunapiga kelele (kama zile za mlango zisizoweza kumkosesha mwenye nyumba usingizi, sasa ana hiyari mwenye nyumba kutengeneza mlango au auache mlango uendelee kumpigia kelele)…tunakejeliwa sana, lakini nataka niwahakikishieni Watanzania kuwa tuna uhakika na tunachokisema, sisi si wendawazimu hadi tuwe tunaropoka mambo ambayo hatuna uhakika nayo,” anasisitiza Dk. Slaa.

Huku akionyesha wazi kuwa na shauku ya ripoti hiyo kuwekwa hadharani ili Watanzania wote wafahamu kilichomo, anasema serikali inapaswa kuiweka hadharani kama ilivyowaahidi wabunge wakati ilipotoa maelezo kuhusu uchunguzi huo.

Lakini pia Dk. Slaa anawakumbusha watawala kuwa wao si waamuzi wa mwisho wa mambo yanayohusu maslahi ya taifa, walichokabidhiwa ni dhamana ya kuwaonyesha watanzania kule wanakotakiwa kwenda na si kuwafanyia maamuzi yote.

Hata hivyo, katika mazingira ya kawaida, Dk. Slaa anaweza kuwa anahatarisha maisha yake kwa sababu anapingana na watu wenye uwezo wa kufanya chochote kutokana na uwezo mkubwa wa kifedha waliojikusanyia.

Ingawa yeye mwenyewe anaonekana kutotishika na ukweli huo, watu wengi sasa wanaonekana kufuatilia zaidi mwenendo wa maisha yake, hasa wananchi wa chini ambao amekuwa akiwaita mawakili wa kesi yake.

“Ndiyo maana nimeamua sasa kuwa kila ninachokifahamu kuhusiana na ufisadi nakieleza hadharani, hivi ninapozungumza na wewe nimetoka kuhutubia mkutano wa hadhara na tangu juzi nafanya mikutano hiyo katika jimbo langu.

“Natumia fursa hiyo kuwaeleza wananchi yote ninayoyafahamu kuhusiana na ubadhirifu na ufisadi ili kama likinitokea lolote, wawe na taarifa zote na wataamua wenyewe cha kufanya,” anasema.

Dk. Slaa alifanya mahojiano haya kwa njia ya simu akiwa jimboni kwake Karatu, baada ya kutolewa kwa taarifa za Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa Ballali kuwa gavana.

Rais alifikia uamuazi huo baada ya ripoti ya uchunguzi uliofanywa na kampuni ya ukaguzi wa hesabu ya Ernst & Young kubaini kasoro kubwa katika akaunti ya malipo ya madeni ya nje (EPA) katika mwaka wa fedha 2005/06.

Katika maamuzi hayo, baada ya kutengua uteuzi wa Dk. Ballali, Rais Kikwete alimteua aliyekuwa Naibu Gavana, Profesa Benno Ndulu, kuchukua nafasi hiyo.

Aidha, Rais alimpa miezi sita Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kwa kushirikiana na Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania (IGP) na Taasisi ya Kupambana na Kuzuia Rushwa (Takukuru) kuendesha uchunguzi dhidi ya wale wote waliohusika na upotevu wa fedha kupitia akaunti hiyo na kuwachukulia hatua.

Hatua zitakazochukuliwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa fedha zote zilizoibwa kupitia EPA zinarejeshwa.

Pia aliitaka bodi ya BoT kufanya vikao na kuwashughulikia wafanyakazi walio chini ya mamlaka yake walioshiriki katika kashfa hiyo ya EPA.

Ili kuhakikisha kuwa EPA haiendelei kuwa mrija wa mapato kwa wajanja wachache, Rais Kikwete alisitisha ulipaji wa madeni kwa kutumia akaunti hiyo mpaka hapo utaratibu mzuri utakapoandaliwa.

Tuesday, January 15, 2008

Ballali Ana Siri Nzito Moyoni

WASIWASI na woga umeanza kuwatesa baadhi ya viongozi serikalini, na wafanyabiashara wakubwa wanaotajwa kuhusika katika kashfa ya upotevu wa mabilioni ya shilingi dhidi ya siri nzito aliyonayo moyoni, aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu (BoT), Dk. Daudi Ballali.
Inaaminika kuwa kokote aliko, Dk. Ballali, ambaye uteuzi wake ulitenguliwa na Rais Jakaya Kikwete mapema wiki hii, anayo siri nzito moyoni mwake, na iwapo atapata nafasi ya kuiweka hadharani, mwenendo wa kashfa hizo unaweza kubadilika na kuharibu kabisa upepo wa kisiasa, utawala na biashara hapa nchini.

Aidha, siri hiyo inaelezwa kuwa ni nzito kiasi kwamba inaweza pia kuwaharibia watu wengi na hata kuchafua kabisa rekodi zao licha ya sifa nzuri walizonazo sasa.

Dk. Ballali ameamua kutumia siri hiyo kama turufu ya kujilinda na kujihakikishia usalama wake dhidi ya tuhuma zinazomkabili.

Ballali analinda siri hiyo kwa hali na mali ili kuhakikisha inamsaidia kabla haijavuja na kwamba ameamua kwenda hatua kadhaa mbele akitumia siri hiyo kama kinga dhidi yake na mtego dhidi ya maadui zake.

Watu walio karibu naye walieleza kuwa, baada ya kuona hali ya mambo imeanza kugeuka, Dk. Ballali aliamua kumtafuta wakili na kuandika maelezo ya kina kuhusu kile anachokifahamu katika sakata zima la akaunti ya madeni ya nje (EPA).

Kwamba katika maelezo hayo, Dk. Ballali ametoa sehemu ya siri hiyo, huku akitaja majina ya kampuni na watu ambao kwa namna moja au nyingine walihusika katika mipango ya sakata zima la upotevu wa fedha za EPA.

Aidha, taarifa hiyo ya Ballali iliyohifadhiwa kwa wakili huyo ambaye hajatajwa, ina maelezo ya kina pia kuhusu watu ambao kwa namna moja au nyingine walikuwa na mkono wao katika maamuzi kuhusu EPA, lakini ushiriki wao huo unaweza usionekane katika uchunguzi wa kawaida.

Baada ya kutoa maelezo hayo, Dk. Ballali ambaye mpaka sasa hali ya afya yake inaendelea kuwa kitendawili, inadaiwa kuwa alitoa maelekezo kwa wakili huyo na watu wengine wa karibu yake, kuhusu wanachopaswa kufanya iwapo atafikwa na jambo lolote ambalo aidha yeye mwenyewe au mtu mwingine wa karibu yake atalitilia shaka.

Dk. Ballali ameelezwa kufanya hivyo kama jitihada zake za makusudi za kuhakikisha kuwa hafanywi kuwa mbuzi wa kafara katika mchezo ambao ulihusisha wachezaji wengi.

Kwamba lengo lake kubwa la kufanya hivyo, ni kutaka kuhakikisha kuwa, baadhi ya watu waliohusika katika mchezo huo hawamtumii yeye kwa aidha kujisafisha kwa namna yoyote ya kujivua madhambi waliyokuwa nayo katika kashfa hiyo na kumvika yeye.

Kasoro zilizobainika katika akaunti ya malipo ya madeni ya nje ndani ya BoT, zilihusisha watu wengi, akiwemo Ballali na wengine anaowafahamu moja kwa moja na wale ambao hawafahamu.

Lakini, baada ya Kampuni ya Ernst & Young kukamilisha ripoti yake na Rais Kikwete kutoa maamuzi, inaonekama kuwa Ballali ndiye alikuwa mchezaji mkuu katika mchezo huo ambao kuibuliwa kwake kumelitikisa taifa na mataifa ya nje.

Hata katika akili ya kawaida, inaonyesha kuwa Dk. Ballali hakuwa peke yake katika suala hili, bali wapo wengine wengi, hususan vigogo kuliko Ballali.

Hayo yanatokea wakati haijawekwa wazi Dk. Ballali yupo katika hali gani au yupo wapi hasa.

Kinachoshangaza, wakati kulazwa kwa gavana huyo wa zamani wa BoT hakukustahili kuwa siri, hakuna aliyekuwa tayari kutoa taarifa za kina tangu alipoondoka nchini kwenda Marekani kutibiwa, takriban miezi minne sasa.

Awali ilidaiwa kuwa, amekwenda Marekani kwa ajili ya uchunguzi wa afya yake lakini alipokuwa huko ikatolewa taarifa kuwa anaumwa na amelazwa. Baadaye kidogo zikaja taarifa kuwa amefanyiwa upasuaji mubwa.

Tangu uteuzi wake ulipotenguliwa, watu wengi wamekuwa wakitaka Dk. Ballali arejeshwe Tanzania na kushitakiwa sambamba na watu wengine watakaobainika kuhusika na kashfa ya EPA.

Dhamira hiyo ya wengi hailengi kuona tu kuwa kiongozi huyo anashtakiwa, bali wanaamini kuwa, akiwa nchini, anaweza kutoa maelezo mengi na ya kina kuhusu EPA na masuala mengine yaliyomo katika kashfa zinazoelekezwa BoT.

Dk. Willibrod Slaa, ambaye ni muasisi wa tuhuma za ubadhirifu BoT, ni mmoja wa watu wanaoamini kuwa Dk. Ballali ana mengi ya kueleza kuhusu ubadhirifu huo.

Dk. Slaa alisema kuwa, yaliyoelezwa na serikali baada ya kupokea ripoti ya uchunguzi wa EPA uliofanywa na Ernst & Young, ni sehemu ndogo tu ya ubadhirifu mkubwa ambao umefanywa na baadhi ya watu waliopo madarakani na wafanyabiashara.

Dk. Slaa alikwemda mbali zaidi kwa kusema kuwa yeye binafsi anafahamu ubadhirifu uliofanywa kupitia kampuni nyingine kama vile Deep Green, Meremeta na Tangold na iwapo serikali itaendelea kuwa na kigugumizi cha kusema kuhusu hayo, itafika siku ataamua kuyaweka hadharani.

Friday, January 11, 2008

Kenya Kuchemka Upya

Mambio yanazidi kuwa mabaya huko Kenya. Baada ya kushindwa kwa juhudi za kidiplomasia kumaliza mgogoro uliokuwepo, sasa chama cha ODM kimeamua kurudi kwa wananchi. Hivi punde kimetoa tangazo kikiwataka wafuasi wake wajiandae kwa maadamano makubwa nchi nzima kupinga ushindi wa Kibaki. Hakuna anayejua ni nini kitatokea, hasa ukizingatia uzoefu wa maandamano ya kwanza ambapo mamia ya watu waliuawa na mali kuharibiwa.
Hali hii inatishia sana usalama hata wa Tanzania kwa sababu upo uwezekano kuwa madhara yake yakawa makubwa, hasa baada ya kuonyeshwa kuwa Tanzania inapoteza mapato mengi kutokana na vurugu nchini Kenya.

Wednesday, January 9, 2008

BREAKING NEWS: JK AMTIMUA BALALI

Sasa Kikwete anaweza kuwa ameamua kukifanya kile ambacho watanzania wengi walitaka akifanye tangu alipoingia madarakani. Habari zinazosambaa sasa hivi ni kuwa amemfukuza kazi Gavana wa benki Kuu na kuagiza watu wote ambao wametuhumiwa katika ripoti ya uchunguzi wa benki Kuu washughulikiwe.
Kama hatua hii haitakuwa na maana ya kuwatoa mbuzi wa kafara (ili kundi kubwa lipone) sasa tutarajie kupanda kwa chati ya rais Kikwete.
lakini ametoa mtihani kwa Mwanasheria mkuu kwa sababu iwapo watalaamu waliochunguza wamebaini ubadhirifu kiasi cha rais kufikia uamuzi wa kumfukuza mtu, itashangaza sana wao watakaposhindwa kuja na kesi ya kumfunga mtu kifungo kirefu

Tuesday, January 8, 2008

POLISI WANATUZUGA?

Akizungumzia tukio la kushambuliwa kwa wahariri wawili wa Mwana halisi, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya dar es Salaam, Kamishna Alfred Tibaigana amesema kuwa watu wawili wamekamatwa. Mmoja wa watu hawa ni mzee wa miaka inayokarinia 70! Mwingine amekamatwa kwa sababu amekutwa na kofia yenye damu! Sijui Polisi wana ushahidi uliowashawishi wawakate watu hawa lakini kama ushahidi wenyewe ndio huu ambao Tibaigana anausema, nina wasiwasi sana kwamba Polisi wanatuzuga.
Itashangaza sana iwapo mzee wa miaka hiyo awe ndiye aliyepambana kijasiri na kufanikiwa kuchomoka na kukimbia.
Na huyu mwenye kofia yenye damu, hivi kama akiwa ni mchinja mbuzi wa kule Vingunguti, polisi wanataka kutushawishi vipi?
Sasa hivi ndio Tibaigana anashituka na kuunda timu ya watu saba, inayioongozwa na yeye mwenyewe kulishughulikia tatizo hili. Sijui kama anafahamu kuwa anachokifanya ni kutibu tatizo ambalo tayari limeshatokea.
Alikuwa na nafasi ya kuzuia jambo hilo lisitokee. Mmoja kati ya walioshambuliwa, saed Kubenea, mara kadhaa ametoa taarifa polisi kuwa alikuwa si tu akipokea ujumbe wa vitisho, bali kulikuwa na majaribia ya kumdhuru.
Tibaigana na watu wake labda walidhani kuwa Kubenea anatafuta umaarufu au vipi? Wakadharau na kumuacha hivihivi mpaka alipopatwa na makubwa. Tunashukuru Mungu kuwa ameanza kuona tena na tunaamini kuwa huko India alikopelekwa, atapatiwa matibabu yatakayomrudishia afya yake kama awali.
lakini hili linafaa kuwa funzo kwa polisi kuwa mtu anapotoa taarifa za kutishiwa maisha yake, ifahamike kuwa maisha yake yapo hatarini. Na kwa kuwa ni kazi ya polisi kulinda raia na mali zake, wanawajibika kuyalinda maisha ya mtu huyo kwa gharama yoyote ile kwa sababu yeye ndiye anayelipa kodi inayowalipa wao mshahara kwa kazi ya kumlinda.

Sunday, January 6, 2008

BREAKING NEWS: WAHARIRI WASHAMBULIWA

Katika kile kinachoweza kuelezewa kuwa ni hujuma mbaya kabisa nchini, wahariri wawili wa gazeti la Mwana Halisi, wameshambuliwa siku ya Jumamosi kati ya saa 3 na saa 4 usiku.
Mhariri Mkuu wa gazeti hilo, Saed Kubenea ndiye aliyeathirika zaidi baada ya kumwagiwa tindikali usoni na taarifa zilizopatikana hivi punde kutoka Hosptali ya taifa Muhimbili alikolazwa, zinaelezwa kuwa amepoteza uwezo wake wa kuona.
Watu hao watatu, ambao mmoja alikuwa na panga, mwingine rungu na mwingine chupa iliyokuwa na rtindikali, waliwavamia wahariri hao ofisini kwao wakati walipokuwa wakiendelea na kazi ya kuandaa gazeti.
Walianza kugonga mlango baada ya kushindwa kuufungua na Kubenea alidhani kuwa ni wageni wa kawaida hivyio aliondoka kwenda kuwafungulia huku akiwataka wagomge polepole lakini alipofungua na kuona zana zao, alirudi ndani kwa kasi akiandamwa na yule mwenye chupa ya tindikali.
Wakati Kubenea akivamiwa na watu hao na kumwagiwa tindikali, Mhariri wa Habari wa gazeti hilo linalotoka mara moja kila wiki, Ndimara Tegambwage, alivamiwa na wale wawili na mmoja akaanza kumshambulia kwa panga.
Katika purukushani hiyo walimjeruhi Tegambwage, ambaye pia huandikia safu ya SITAKI katika gazeti la Tanzania Daima Jumapili.
Inaweza kuwa ni ajali ya kawaida lakini mazingira yake yanatia shaka kubwa sana. Tangu lianzishwe, Mwana Halisi limejidhihirisha katika jamii kama gazeti ambalo lipo mstari wa mbele kufumua na kuandika maovu yanayofanywa na viongozi kadhaa.
Gazeti hilo limejijengea sifa ya kutomung'unya maneno pale linapokuwa na habari fulani. Habari zake huandikwa kwa kutaja kila kitu pamoja na majina halisi ya wahusika. lakini kutokana na ujasiri huo, Mwana Halisi, wahariri na waandishi wake wamejijengea uadui na kundi fulani la watu na vitisho kwao viligeuka kuwa suala la kawaida.
Kubenea na Tegambwage labda hawakuwa na habari kuwa waliokuwa wakiwatishia walikuwa wanaandaa nini mkapa maswahibu haya yalipowakuta.
Wakati tunawaombea Kubenea na Tegambwage, ni wakati wa kuangalia waaandishi wanafanya nini ili kujilinda dhidi ya njama na hujuma kama hizi.

Bei ya mafuta kukwaza uchumi 2008

SASA watanzania wanapaswa kujiandaa na hali ngumu itakayotokana na kushindwa kukua kwa uchumi kwa kasi ambayo ilitarajiwa kuleta nafuu katika maisha.

Kudumaa kwa hali ya uchumi kutatokana na kuongezeka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia, jambo ambalo mara kadhaa Rais Jakaya Kikwete amekuwa akilielezea kama moja ya sababu kubwa zinazoikwamisha serikali yake kutekeleza kwa kasi ahadi ya kumletea kila mtanzania maisha bora.

Kwamba kupanda kwa bei ya mafuta ni kidonda kwa uchumi wa nchi inathibitishwa na ukweli kuwa bajeti ya serikali ya mwaka 2007/08, iliyopitishwa mwezi Agosti mwaka jana, haikufikiria wala kuweka tahadhari ya kukua kwa bei ya mafuta kama moja ya matatizo ambayo yanaweza kusababisha matatizo katika utekelezaji wa bajeti.

Licha ya kutoweka tahadhari hiyo katika bajeti, pia mipango ya nchi kuhusiana na uchumi, tangu kuanza kwa mageuzi ya kiuchumi, haijawahi kufikiria bei ya mafuta kama kigezo muhimu katika upangaji wa mipango hiyo.

Licha ya kuwa suala la bei ya mafuta linafahamika kwa wataalamu wanaoandaa mipango ya uchumi wa nchi, hakuna sehemu katika mipango hiyo panapoonyesha jinsi nchi ilivyojiandaa kukabili kikwazo hicho.

Suala la bei ya mafuta limekuwa likitajwa tu kama tatizo linaloikwamisha serikali ambayo viongozi wake wengi, akiwamo rais Kikwete, wanaishia kusema kuwa serikali haina lolote la kufanya kuhusiana na bei hiyo.

Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi ya utafiti wa uchumi ya ESRF, Dk. Lunogelo Bohela, ameniambia kuwa upangaji wa mipango kama vile MKUKUTA, MKURABITA na mingineyo, haukuzingatia bei ya mafuta kama moja ya vikwazo vinavyoweza kukwamisha utekelezaji wake.

Katika mahojiano nami, Dk. Bohela alibainisha kuwa huo ni upungufu mkubwa katika masuala ya uchumi, kwani athari za bei ya mafuta kwa uchumi wa nchi kama Tanzania, ambayo inategemea nishani hiyo katika uzalishaji, ni kubwa sana na ilipaswa kutiliwa maanani.

“Hadi hivi sasa bado tunategemea mafuta kama nishati ya msingi ya uzalishaji, tunatumia umeme kwa kiasi fulani lakini hata huo umeme nao sehemu yake unazalishwa kwa mafuta, hivyo tutake tusitake bado mafuta yataendelea kuwa ndio msingi wa uchumi wetu,” alisema.

Dk. Bohela alisema kuwa ilitarajiwa kuwa gesi asilia ingesaidia kupunguza utegemezi wa mafuta lakini haijafanya hivyo kwa sababu hivi sasa bado uwekezaji katika eneo hilo haujafikia kiwango kikubwa.

Akielezea matarajio yake kuhusiana na kufikiwa kwa malengo ya kukua kwa uchumi yaliyowekwa, baada ya bei ya mafuta kufikia rekodi ya dola za Marekani 100 kwa pipa na kutoonyesha dalili za kupungua, Dk. Bohela alisema kuwa itakuwa vigumu sana kwa Tanzania kufikia malengo hayo mwaka huu.

“Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita bei ya mafuta imeongezeka maradufu… inavyoonekana ni kuwa bei haiwezi kupungua, itandelea kupanda tu na hii itatuathiri sana.

“Sana sana, iwapo tutajitahidi kuchukua tahadhari kuzuia athari za kupanda kwa bei mafuta, tunachoweza kufanya ni kuhakikisha kasi ya kukua kwa uchumi ina-stabilise (inabaki kama ilivyo), yaani ibakie ileile ya mwaka uliotangulia, lakini sina matarajio makubwa sana kuwa tutaweza kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi katika hali hii,” alisema.

Dk. Bohela, ambaye ni mtaalamu wa uchumi katika nyanja ya kilimo, alisema kuwa kungekuwa na nafuu kubwa iwapo nchi ingekuwa inategemea malighafi nyingi kutoka nchini.

Alisema kuwa iwapo viwanda vinavyozalisha bidhaa nchini vingekuwa vinatumia malighafi nyingi za ndani, hiyo ingepunguza gharama za uzalishaji na kufanya bei ya bidhaa zinazozalishwa kuwa ya chini na kuleta unafuu kwa walaji.

“Hii gharama ya uzalishaji ndiyo kimsingi inayosababisha kupanda kwa mfumko wa bei za bidhaa… tuna bahati mbaya kwamba tunategemea nishati ya mafuta kutoka nje na pia malighafi kutoka nje,” alisema.

Akifafanua madhara ya kupanda kwa bei ya mafuta, alisema kuwa licha ya kuongeza gharama za uzalishaji, lakini kupanda kwa bei ya nishati hiyo kutaongeza pia gharama za usafiri na usafirishaji.

Akitoa ushauri, Dk. Bokela alisema serikali inaweza kuanzisha mazungumzo na moja ya nchi marafiki zinazozalisha mafuta na kukubaliana bei maalum ya upendeleo ambayo Tanzania itakuwa ikuziwa.

“Hii imeshawahi kufanyika huko nyuma na nadhani inaweza kufanyika hivi sasa kwa sababu tutaumia sana iwapo tutaendelea kutegemea mafuta kupitia soko la dunia,” alisema.

Mara kadhaa, rais Kikwete ameelezea kupanda kwa bei ya mafuta katika soko la dunia kama moja ya sababu zinazoikwamisha serikali kutekeleza mipango yake ipasavyo.

Katika hotuba zake, Kikwete husema kuwa bei ya mafuta katika soko la dunia imeiweka serikali kwenye hali mbaya kwa sababu haina uwezo wa kufanya lolote kuhusiana na udhibiti wa bei hiyo.

Wednesday, January 2, 2008

Uchaguzi Kenya na Mustakabali wa EAC

Uchaguzi Kenya na mustakabali wa EAC

Wakati wa ukusanyaji wa maoni kuhusu haja ya kuharakisha uundwaji wa Shirikisho la Afrika Mashariki, asilimia 75 ya watanzania walipinga wakisema hakukuwa na haja ya kuharakisha uundwaji wa shirikisho. Katika hao waliopinga, wapo waliohusisha hali ya amani na utulivu katika nchi za Kenya na Uganda na kueleza wasi wasi wao kuwa huenda ikaathiri shirikisho hilo.

Walitilia wasiwasi hali na mifumo ya kisiasa na kueleza kuwa haiendani na hali na mifumo ya kisiasa inayofuatwa na Tanzania. Baadhi ya viongozi waliwabeza wananchi hawa, wakisema kuwa hiyo ni hofu tu.

Walihakikisha kuwa hali ya kisiasa katika nchi hizo si sababu ya kuhofu. Lakini viongozi na wananchi wa Kenya wameamua kuonyesha kwa vitendo kuwa hofu hiyo iliyoonyeshwa na watanzania wengi na kuopuuzwa na badhi ya viongozi ni hofu halisi ambayo inapaswa kzuingatiwa kwa makini.

‘Sarakasi’ zilizofanywa katika uchaguzi mkuu wa Kenya hadi hivi sasa zimesababisha vifo vya zaidi ya watu 160. na hakuna anayejua kuwa idadi hiyo ni halisi au la kwa sababu hali ya mawasiliano imekuwa ngumu kiasi kwamba kuna uwezekano wapo wengi waliokufa lakini hawajatambuliwa.

Katika hatua iliyofikiwa nchini humo kutokana na uchaguzi mkuu, ni rahisi kumlaumu kila mtu. Lakini kwa ujumla, viongozi wa serikali na upinzani, wanasiasa na wananchi, wanapaswa kubeba lawama kutokana na machafuko yaliyotokea.

Wanachopigania ni matokeo ya uchaguzi. Wakati rais Kibaki, serikali yake pamoja na chama chake cha PNU wanatangaza kuwa wameshinda kihalali (sijui kama wanaamini hivyo), wapinzani, wakiongozwa na raila odinga wa ODM, wanadai kwa nguvu kuwa wameporwa ushindi wao.

Mabishano haya ndiyo yaliingiza wananchi mitaani, hasa baada ya kuapishwa kwa Kibaki, dakika chache tu baada ya kutangazwa kwa matokeo katika mazingira ya kutatanisha.

Polisi, waliotakiwa kulinda usalama, waliwapiga watu risasi katika kile kinachoelezwa kutuliza ghasia. Habari zilizopo zinaonyesha kuwa polisi hawakushambuliwa na silaha za moto na watu waliokuwa wanafanya fujo. Ni sehemu moja, Kisumu, ambako inaelezwa kuwa polisi waliwapuiga risasi wananchi wlaiowarushia mawe.

Inashangaza kuwa wakati wana zana nyingi za kutuliza ghasia bila kulazimika kupiga risasi za moto, polisi wanawesza kujibu mashambulizi ya mawe kwa risasi za moto!

Kwa upande mwingine, Odinga anafahamu kuwa ana wafuasi wengi nchini humo. Huu ni mtaji wa kisiasa ambao ameamua kuutumia kufikia malengo yake, kuwa kiongozi wa Kenya. Inatia moyo kuwa anahubiri amani, akiwataka wafuasi wake kuacha kufanya fujo na kuwa watulivu.

Lakini wakati huo huo, anawahimiza kushiriki katika maandamano ya amani kushinikiza Kibaki aachie ngazi. Odinga ameshawajaza wafuasi wake ujumbe kuwa kura zai zimeibwa, na anajua wazi kuwa katika mazingira ya siasa za mgawanyika kama zilizopo Kenya, haiwezekani kwa wafuasi wake kuwa wartulivu huku wakifahamu fika kuwa kura zao zimehujumiwa.

Hawawezi kuwa watulivu hasa bada ya msimamo na tabia zinazoonyeshwa na Kibaki, chama chake na serikali yake. Jinsi anavyong’ang’ania madaraka wakati ushahidi uliopo unaonyesha kuwa ushindi wake ni wa kupikwa.

Wafuasi wa Odinga hawawezi kutulia sasa wakati baadhi ya Tume ya Uchaguzi (ECK) wameanza kutoa maelezo yanayozidi kuthibitisha kuwa matokeo yaliyotangazwa yalikuwa na mushkeli.

Wajumbe wanne wa tume hiyo waliwaambia waandishi wa habari kuwa kuna umuhimu wa kuunda chombo kingine huru kuchunguza kile kilichotokea kwa sababu inavyoonekana kuna kasoro nyingi katika ujumlishaji wa matokeo.

Hata kama mwenyekiti wa ECK, Samuel Kivuitu atajitokeza kukanusha taarifa hizo, bado haitaondoa ukweli kuwa wajumbe hao wameongezea tu kwenye kasoro ambazo zilishaelezwa awali na waangalizi wa uchaguzi huo kutoka nje na ndani ya Kenya.

Serikali imeaanza jitihada za kutuliza hali ya mambo. Lakini inachokifanya hakiwezi kufanikiwa kwa sababu mazingira yanaonyesha wazi wazi kuwa ushindi wa Kibaki una kila aina ya dosari, si halali.

Katika mazingira hayo, Odinga, ambaye amekuwa akiipigania nafasi hiyo kwa miaka mingi, hawezi kukubaliana na ameshaonyesh hilo. Inafahamika kuwa mazungumzo ndio njia bora zaidi ya kumakliza tofauti baina ya watu wanaopingana. Kutokana na vurugu hizo, Odinga aliombwa kukutana na Kibaki ili kuzungumza na kumaliza tofauti zilizojitokeza.

Sharti kubwa alilolitoa ni kuwa Kibaki ajiuzulu kwanza na ndipo atakapokaana naye mza moja na kujadili. Anasema kua kukaa na Kibaki wakati akiwa bado anashikilia wadhifa wake wa urais, ni sawa na kukubali kuwa ameshinda kihalali wakati yeye (Odinga) anaamini kuwa Kibaki hakuingia madarakani kihalali.

Haya yanakumbushia yaliyowahi kutokea Zanzibar katika chaguzi. Mara zaote, Chama cha Wananchi (CUF) kimekuwa kikitoa madai baada ya uchaguzi kuwa kimeporwa ushindi. Jitihada zilifanywa kila mara kuwaleta CUF kaatika meza ya mazungumzo pamoja na mshindi. Lakini mara zote, CUF wamekataa kwa kusema kuwa kukaa meza moja na mtu huyo, ni sawa na kukubali ushindi wake.

Kilichotokea katika mabishano hayo bado ni kidonda ambachio kinaiumiza Tanzania hadi hivi leo. Katika uchaguizi wa mwisho, rais Abeid Aman karume aliapishwa saa chache tu baada ya matokeo kutangazwa kama ambavyo Kibaki ameapishwa dakika chache tu baada ya kutangazwa kwa matokeo.

Kama ilivyowahi kutokea kwa Zanzibar, mtiririko wa matukio katika uchaguzi unafanana na wa Kenya. Kila chama kilianza kujitangazia matokeo yake mapema huku tume ya uchaguzi nayo ikitoa matokeo yake. Inapofika wakati fulani karibu na mwisho, kama ambavyo CUF na CCM waliandika kwa tume ya uchgauzi kulalamikia matokeo, ODM na PNU nao walilalamika kwa tume kuwa wananyongwa.

Polsii na vikosi vya usalama vilitumika kuhalalisha matokeo ya uchaguzi zanizbra kama ambavyo sasa polisi na vikosi vya usalama vinavyotumika kuhalalisha ushindi wa Kibaki Kenya.

Lakinimkuna tofauti kubwa. Wananchi wa Kenya inaonekana wana mwamko mkubwa. Inaweza kuwa mwamko huo umejengwa kutokana na ukabila wao na watu wa kabila fulani wanaamua kulinda maslahi ya mgombea wa kabuila lao. Lakini kinachoonekana ni mwamko wao wa kutokubali kuibiwa.

Hali hii ni tofauti na watanzania ambao ishindi wa chama cha siasa hauna maana sana kwao kiasi cha kuwa tayari kupoteza maisha wakiutetea.

Na hiki ndicho walichokuwa wakikielezea watu waliokuwa wakipinga uharakishwaji wa uundwaji wa shirikisho la Afrika Mashariki, ingawa hakukieleweka wakati ule.

Watanzania wanauogopa mwamko huo wa wakenya wa kuwa tayari kupoteza maisha kwa ajili ya ushindi wa kiaisa. Wanaogopa kwa sababu hawajaiona mipaka ya mtu huyo aliye tayari kufa kwa ajili ya siasa. Wanajiuliza mpaka hivi sasa, kama yupo tayari kufa kwa ajili ya siasa, ambayo haina uhusiano wa moja kwa moja na kuleta sahani ya ugali mezani kwake, atafanya nini katika suala linalohusiana moja kwa moja na maisha yake, kwa mfano ajira.

Wakati wakenya wameonyesha kwa vitendo kuwa hofu ya watanzania kuhisna na siasa za Kenya ni halisi, inakuja changamoto nhingine. Pamoja na yanayotokea Kenya, bado dhamira ya kuunda Shirikisho la Afrika mashariki itaendelea.

Lakini, matukio haya yamethibitisha hofu ya watanzania na nidhahiri kuwa yatakuwa ni rejea pale ambapo watanzani watatakiwa kufikiri tena kuhusiana uundwaji wa shirikisho.

Wakati tunafikiri jinsi ya kuisadia Kenya kumaliza changamoto za uchaguzi wake mkuu, inapaswa tufikirie pia athari ya yaliyotokea katika dhamira yetu ya kuunda shirikisho la Afrika Mashariki. Tutafanya makosa makubwa iwapo tutaamua kufunika kombe ili mwanaharamu apite.

Huyo mwanaharamu hatopita, na kama akipita hatokwenda mbali, na atarudi kuja kutuandama. Hivyo ni uamuzi wetu iwapo tumshughulikie sasa hivi au tuendelee kuahirisha tatizo.